Wakati Serikali ikijiandaa kushirikiana
na ya sekta binafsi katika usajili wa vikundi vyote vya ujasiriamali ili viweze
kufanya kazi kwa mujibu wa sheria na taratibu za Nchi, Wananchi na hasa Vijana
wanapaswa kuitumia fursa hiyo kwa kupata ajira ambazo uwezo wa serikali
wa kuwaajiri kwa wakati huu ni mdogo.
Wito huo umetolewa na Makamu wa Pili wa Rais
wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akiyafungua maonyesho ya siku mbili ya
wajasiri amali ikiwa ni shamra shamra za maadhimisho ya siku ya Wanawake
Duniani yanayofanyika katika bustani ya Mnara wa Kumbu kumbu ya Mapinduzi
uliopo Muembe Kisonge Michenzani Mjini Zanzibar.
Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali kupitia
Mfuko wa uwezeshaji iko tayari kuwadhamini wajasiri amali watakaofuzu mafunzo
yao yanatolengwa kutolewa katika Wadi na shehia zote za Unguja na Pemba.
Alisema Taifa linaelewa changamoto
zinazowasumbua wajasiriamali zikiwemo ukosefu wa mafunzo ya mara kwa mara,
mitaji midogo pamoja na maeneo ya kufanyia biashara zao mambo ambayo
yanachangia upatikanaji mdogo wa ufanisi wa kazi zao.
Balozi Seif alieleza kwamba changamoto hizo
zitafanyiwa kazi na Serikali ili kuiwezesha sekta hiyo binafsi ya
ujasiria amali kuwa kimbilio kwa vijana walio wengi hasa ikizingatiwa uhaba wa
nafasi za ajira uliopo Serikalini.
Alifahamisha kwamba Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar inatambua wazi kuwa wajasiriamali ni nguzo imara ya uchumi wa
Taifa ikielewa kuwa sekta hiyo ndio mkombozi wa wananchi walio
wengi hapa nchini.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
ameishukuru Benki ya Posta Tanzania, Benki ya Wakulima Vijijini { CRDB } pamoja
na mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar {ZSSF} kwa mchango wao wa kusaidia
wajasiriamali katika kutatua matatizo yao ya ukosefu wa mitaji ya kuendesha
miradi yao.
Alisema mchango wa Taasisi hizo za kifedha
umedhihirisha wazi jinsi zinavyothamini nguvu za Wananchi wao wenye
juhudi za kujikwamua kimaisha kwa kujishughulisha na kazi halali za kujiongezea
kipato.
Balozi Seif aliwapongeza waandaaji wa
maonyesho hayo ya wajasiriamali yenye kuvutia ambayo yatawasaidia kuwaelimisha
wale waliokuwa wazito wa kujielekeza katika jeshi hilo kubwa la
wajasiriamali hapa Nchini.
Mapema Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Posta
Tanzania Bwana Sabasaba Moshing alisema katika kupiga vita umaskini
unaooneka kuiathiri jamii kubwa Nchini Taasisi hiyo ya kifedha inaendelea kutoa
mikopo kwa wajasiriamali kwenye maeneo mbali mbali nchini kwa lengo la
kukabiliana na tatizo hilo.
Bwana Sabasaba alisema Benki ya Posta
Tanzania tayari imeshafungua Akauni Elfu 4,000 za vikundi vya vikoba na akauni
nyengine 1,000 kwa vikundi visivyo rasmi kutekeleza azma ya Benki hiyo tokea
ilipoanzishwa kwake kwa nia ya kumkomboa mwananchi.
Akitoa salamu Mwenyekiti wa Taifa wa
Shirikisho la wajasiriamali Tanzania { TISF } Bwana Masoud Hassan Maftaha alisema Taasisi hiyo inatoa siku 60
kuanzia leo kuendesha mafunzo bure yatakayowajengea uwezo wa kitaaluma
wajasiria amali wa Zanzibar.
Bwana Masoud alisema Tanzania sio omba
omba iwapo mipango imara itadumishwa katika kuwajengea uwezo
wananchi wake hasa wale walioamua kujikita katika sekta ya ujasiriamali.
Mwenyekiti huyo wa Taifa wa Shirikisho la
wajasiriamali Tanzania alifafanua kwamba wajasiriamali wa Zanzibar lazima
wawezeshwe ili kukidhi mahitaji yao muhimu pamoja na kwenda sambvamba na
mpango huo.
Akimkaribisha mgeni rasmi kwenye uzinduzi wa
maonyesho hayo ya Wajasiri amali Waziri wa Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana,
Wanawake na Watoto Mh. Zainab Omar Mohammed alisema zipo taasisi nyingi zisizo
za Kiserikali zilizoanzishwa Zanzibar ambazo tayari zimeshaleta faraja
kubwa katika kumkomboa Mwananchi hasa Mwanamke.
Waziri Zainab aliwataka Wananchi hasa Wanawake
na Vijana kuzichangamkia kwa haraka fursa zote zinazotolewa na taasisi hizo ili
kukabiliana na ukali wa maisha na kupunguza umaskini.
Tanzania hivi sasa ina wanachama wa vikundi
vya ujasiriamali wapatao Milioni 7,284,000 kati ya hao wanachama Laki 100,000
na vikundi vilivyosajiliwa vipatavyo Elfu 1,213 vipo Visiwani Zanzibar.
Utafiti uliofanya ndani ya vikundi vya
wajasiriamali nchini umebaini kuwa wajasiri wengi wanafanya biashara zao
chini ya kiwango kinachokubalika cha mtaji, ukosefu wa maeneo ya kufanyia
biashara hizo pamoja na elimu duni ya kuendesha miradi wanayoianzisha.
Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la wajasiriamali Tanzania Zanzibar
Bibi Nuru Mohammed akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa maonyesho
ya wajasiriamali hapo Michenzani.
|
0 comments:
Post a Comment