Zanzibar ni miongoni mwa nchi zenye
kutegema mazao ya kilimo katika kujenga uchumi wake. Wakati Zanzibar
ikiwa inategemea zao la karafuu katika kukuza uchumi wake, nchi kama vile Ivory
Coast inategemea Kokoa na Kahawa, Ghana inategemea Kokoa, Ethiopia Kahawa,
Uganda Kahawa, Kenya kahawa na Chai, Tanzania Bara inategemea Kahawa, Korosho
na Chai.
Nchi ambazo zinategemea zao la
karafuu kama ilivyo Zanzibar kwa kuwa sehemu ya pato la nchi na kukuza uchumi
wake ni pamoja Indonesia, Madagascar, Comoro, Sri Lanka, Brazil na
India.
Sifa na Ubora wa mazao ya kilimo cha
biashara katika kukuza uchumi ni kulinda ubora wa mazao hayo. Mazao yenye sifa
ya ubora ndio yenye bei nzuri katika soko la ndani na nje. Sifa na Ubora
ni kielelezo cha kulinda na kudhibiti mazao hayo katika soko la ndani na nje.
Nchi nyingi zimepitia katika hatua
mbali mbali za Mageuzi katika uimarishaji wa Sekta za Kilimo ili kuzifanya
sekta hizo kua endelevu kwa maslahi ya nchi na wananchi wake.
Baadhi ya nchi, kilimo cha zao la
karafuu hakikupewa kipaumbele sana kutokana na kuwa mchango wake katika
jitihada za kukuza uchumi wa nchi husika ni mdogo.
Zanzibar - imetoa kipaumbele kwa zao
la karafuu kwa kulifanya kuwa sekta inayomilikiwa na Serikali kutokana na
mchango wake mkubwa katika kuimarisha uchumi.
Indonesia - Serikali inasimamia kwa
karibu sana zao la karafuu kwa kuchukua hatua mbali mbali za kurekebisha kasoro
zinazoonekana kuleta athari kwa zao hilo. Usimamizi huo ndio ulioleta
mafanikio ya kuwa wazalishaji wakubwa na ndio wanaongoza duniani.
Madagascar - ni jitihada za Wakulima
wenyewe wanazozifanya ili kujiongezea kipato ila wanahakikisha suala la ubora
wa karafuu zao linazingatiwa na linakuwa ndio kigezo cha ongezeko la thamani ya
karafuu na kipato chao.
Comoro- Wao ni jitihada za Wakulima
wenywe za kujiongezea kipato lakini juhudi zao zimekuwa zikizaa matunda kwani
zimeifanya nchi hio kuwa ya nne (4) katika uzalishaji wa karafuu duniani.
India – Wakulima wanajitegemea
wenyewe, na zao hilo hushuhgulikiwa na matajiri kwani kushughulikia kilimo cha
mikarafuu ni kazi inayohitaji kujituma na uwezo wa kifedha.
Sri-Lanka – Inafahamika kwa
uzalishaji wa viungo (spices) zikiwemo karafuu. Kwa ujumla nchi hii
inasafirisha asilimia 56 (56%) ya viungo vinavyosafirishwa nje, inaingiza fedha
za kigeni asilimia 80 (80%). Kwa kiasi kikubwa Serikali
inashughulikia mageuzi ya sekta hii hasa katika kudhibiti na kulinda ubora.
Mageuzi ya Sekta za Kilimo ndio
yanayotoa mabadiliko ya mfumo wa uendelezaji, uimarishaji na usimamizi wa sekta
za mazao ya kilimo katika nchi ambayo nayo hutegemea Sera za Biashara za nchi
hizo.
Zanzibar inatekeleza mageuzi kwa kuiimarisha sekta ya
karafuu ili iwe endelevu na yenye kuleta tija kwa nchi na wananchi wake
kutokana na karafuu kuwa ni zao lenye faida kubwa.
Nia ya Serikali kwa zao hili ni kuwa
endelevu na lenye kuleta tija zaidi kwa Wananchi ndio maana Shirika la Biashara
la Taifa Zanzibar (ZSTC) limekuwa likichukuwa jitihada kubwa katika kuimarisha
zao hilo na kulinda ubora.
Kwa lengo la kuhamasisha wakulima kulinda ubora wa zao la
karafuu Shirika la ZSTC limeanzisha mpango maalum wa kuwazawadia wauzaji bora
wa zao hilo, kila Wilaya ni lazima apatikaneMuuzaji mmoja bora ambapo
huzawadiwa fedha taslim.
Je ni zipi Sifa za Muuzaji Bora wa zao la Karafuu?
Mkurugenzi wa Mfuko wa Maendeleo ya Karafuu Ali Suleiman
Mussa na Mkurugenzi Masoko wa Shirika la ZSTC- Zanzibar Salum Abdalla Kibe
wamelezea kwa undani sifa na vigezo vya Muuzaji bora wa karafuu na umuhimu wa
kulinda ubora wa zao la karafuu.
Uuzaji mwingi wa Karafuu
Muuzaji bora ni lazima awe ameuza karafuu nyingi kulinga na
kumbukumbu za manunuzi za Shirika la ZSTC katika Wilaya husika aliyopo Mkulima.
Lengo la kigezo hichi ni kuwashajihisha Wakulima kuitikia wito wa Serikali
wa kuziuza karafuu zote katika vituo vya Shirika la Biashara la Taifa (ZSTC) na
kuachana kabisa kuuza kwa magendo.
Kwa upande wake, Serikali imekuwa
ikiahidi kuendelea na azma yake ya kuwapa Wakulima bei nzuri kila bei ya
karafuu inapopanda kwenye soko la dunia na kuwalipa pesa zao taslim bila ya
kuwakopa na bila ya kuchelewa.
Awe mmiliki wa Shamba au kukodi
Muuzaji bora ni lazima awe anamiliki shamba/mashamba au awe
anakodi mashamba kwa njia za halali/kisheria. Lengo la kigenzo hichi ni kuweka
haki, usawa na uadilifu katika bishara hii ya zao la karafuu.
Pia kigezo hichi kinaondoa tabia ya baadhi ya watu kununua
karafuu mitaani kwa njia zisizokuwa rasmi ‘vikombe’ na kuondoa tabia ya wizi na
ukataji wa mikarafuu mashambani kutokana na kuzoeleka kwa biashara hiyo ya
ununuzi wa karafuu mbichi.
Watu wanaofanya biashara hiyo ‘Vishoka’ hawazingatiwi na
Shirika la ZSTC na wala hawafahamiki kisheria, ni Shirika la ZSTC pekee
lililopewa mamlaka ya kununua na kuuza karafuu.
Awe anaanika vizuri kwa kutumia vifaa vinavyotakiwa
Muuzaji bora wa karafuu ni yule anaezingatia ubora wa
karafuu zake kwa kuanika vizuri, katika sehemu nzuri na safi. Awe anatumia
majamvi kwa kuanikia, jamvi ni kifaa pekee kinachaoshauriwa na Shirika la ZSTC
kutumika kwa kuanikia karafuu.
Karafuu zilizoanikwa vizuri kwa kutumia majamvi huwa na sifa
nzuri za ubora kama vile kukauka vizuri, rangi nzuri ya kahawia, haitoki
vichwa, harufu nzuri ya kuvutia na mara zote huwa ni daraja la kwanza ambapo
mkulima hupata fedha nzuri.
Zifa hizo nzuri za ubora huwa haiwezekani kupatikana kwa
karafuu zinazoanikwa barabarani, juu ya mabati na sakafuni ingawa baadhi ya
Wakulima wanaanika katika sehemu hizo. Watu hao hawawezi kuwa bora kwa sababu
wanahatarisha ubora wa zao la karafuu katika soko la nje na kushusha thamani
yake.
Karafuu ziwe zinakauka vizuri kwa kiwango kinachotakiwa
Kwa mujibu wa viwango vya ukaukaji wa karafuu kwa Shirika la
ZSTC, karafuu zinatakiwa zikauke vizuri na zisiwe na unyevu unaozidi aslimia 14
(14%). Kwa mujibu wa kiwango hicho Mkulima anatakiwa ahakikishe karafuu zake
zinapata jua la kutosha sio chini ya siku tatu.
Wakulima wanapopeleka karafuu zao katika vituo vya manunuzi
wakati zikiwa hazijakauka inavyotakiwa hupelekea usumbufu vituoni kwa kutakiwa
kuanika tena na kama zikinunuliwa na kuhifadhiwa katika maghala karafuu hizo
hupugua uzito kwa kiwango kikubwa na hata wakati mwengine kufanya ukungu.
Karafuu zake zinatakiwa kuwa safi
Muuzaji bora lazima azingatie suala la usafi wa karafuu
zake, karafuu hizo zisiwe na vitu visivyohitajika. Kwa mujibu wa vigezo vya Shirika
la ZSTC karafuu hazitakiwi ziwe na taka zinazozidi asilimia 4 (4%).
Kwa bahati mbaya wapo baadhi ya watu huwa wanachafua karafuu
zao kwa makusudi kwa kuingiza unga wa makonyo kwa lengo la kuongeza uzito na
wengine huanika barabarani ambapo karafuu hizo huchafuka kwa kuingia kokoto,
lami, moshi wa magari na ushafu mwengine.
Uhuhimu wa kulinda ubora wa zao la karafuu
Kulinda ubora huongeza thamani ya zao la karafuu katika soko
la nje na kupata bei nzuri. Serikali ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha
mpango wa kuipandisha hadhi karafuu ya Zanzibar kutokana na sifa zake za
kipekee kupia mradi wa ‘Brading’.
Zanzibar sio nchi pekee inayozalisha zao la karafuu, kuna
nchi nyengine kama vileIndonesia, Madagascar, Comoro,
India, Sri-Lanka na Brazil nazo zinazalisha karafuu. Kulinda ubora kunapelekea karafuu za
Zanzibar kuhimili ushindani katika soko la nje.
Zao la karafuu ni zao la uchumi wa nchi na ni zao la
biashara hivyo linahitaji masoko ya uhakika ndani na nje ya nchi. Kulinda ubora
kunasaidia sana kukaribisha masoko mapya ya zao la karafuu.
Ni vyema Wakulima wa zao la karafuu wakatumia fursa ya
mpango wa Shirika la ZSTC la kwazadia Wauzaji bora kuimarisha zao la karafuu
kwa kulinda ubora wa zao hilo ili kuwa na uhakika wa soko na kuongeza tija.
“Karafuu ni Uhai, Karafuu kwa Maendeleo ya Zanzibar”.
Ali Mohamed ZSTC
0 comments:
Post a Comment