February 24, 2016

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 Zanzibar                                                                                                                                 24.2.2016
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisistiza haja ya kuimarishwa uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Kuwait hasa katika kushajihisha sekta ya uwekezaji.
Dk. Shein aliyasema hayo leo huko Ikulu mjini Zanzibar, wakati alipofanya mazungumzo na Balozi Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Kuwait Mhe.  Dk. Mahadhi Juma Maalim ambaye anakuwa Balozi wa mwanzo katika Ubalozi mpya wa Tanzania nchini Kuwait.
Katika mazungumzo hayo Dk. Shein alimueleza Balozi huyo Mteule kuwa Tanzania ikiwemo Zanzibar inajivunia uhusiano na ushirikiano uliopo hivyo iwapo sekta ya uwekezaji itapewa kipaumbele baina ya nchi mbili hizo mafanikio makubwa yanaweza kupatikana.
Aidha, Dk. Shein alipongeza juhudi zinazochukuliwa na Kuwait katika  kuendelea kuiunga mkono Tanzania katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo.
Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa kutokana na hatua kubwa zilizofikiwa katika kuimarisha sekta ya utalii hapa nchini ipo haja kwa nchi hiyo kuendeleza uhusiano na ushirikiano katika sekta hiyo muhimu ambayo inaipatia fedha nyingi za kigeni Tanzania ikiwemo Zanzibar.
Alieleza kuwa Tanzania ni nchi ambayo imejaaliwa kuwa na vivutio mbali mbali vya utalii zikiwemo mbuga za wanyama kwa upande wa Tanzania Bara pamoja na fukwe zenye kuvutia kwa upande wa Zanzibar ambavyo vimeweza kuwavutia wageni wengi kuja kuitembelea Tanzania.
Pia, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumueleza Balozi Mahadhi azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya ajira kwa vijana na kueleza haja kwa nchi hiyo kuimarisha mashirikiano katika sekta hiyo.
Sambamba na hayo, Dk. Shein alimtakia heri na fanaka kubwa Balozi Mahadhi katika utendaji wake wa kazi kwenye Ubalozi huo mpya wa Tanzania nchini Kuwait na kueleza kuwa kwa vile anatambua utendaji wake wa kazi ana matumaini makubwa kwa balozi huyo na Ubalozi huo kuweza kupata mafanikio na kuendelea kuijengea hadhi kubwa Tanzania Kitaifa na Kimataifa.
Nae Balozi huyo Mteule wa Tanzania nchini Kuwait kwa upande wake alitoa pongezi kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza Mapinduzi Dk. Shein pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli kwa kupata uteuzi huo mpya ambapo kabla ya uteuzi huo alikuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Dk. Mahadhi alimuhakikikishia Dk. Shein kuwa katika wadhifa wake huo mpya juhudi za makusudi atazichukua kwa mashirikiano ya pamoja katika kuhakikisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Kuwait na Tanzania unaimarishwa zaidi sambamba na kuimarisha maslahi kwa pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.



Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

0 comments:

Post a Comment