February 05, 2016

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi amesema Vijana wanapaswa kuelewa kazi kubwa ya chama cha siasa ni kushinda uchaguzi ili kushika Dola kama inavyoelezwa katika Katiba na kanuni za Chama cha Mapinduzi.
Akilifungua Kongamano la Vijana wa CCM wa vyuo Vikuu kuadhimisha  miaka 39 tangu kuzaliwa kwa CCM  Mjini Zanzibar amesema Viongozi pamoja na Wanachama hicho CCM wanataka kuona Chama kinaendelea kubakia kuwa kimbilio la Wanawake.
Amesema Chama chochote kitakachojenga tabia ya kudharau kundi la Wanawake ambalo ndio kubwa katika Jamii hakitokuwa na nafasi ya kushinda  uchaguzi kwa sasa na hata hapo baadaye.
“ Wanawake ni zaidi ya nusu ya Watanzania. Sasa ukilidharau kundi hili maana yake umejidharau mwenyewe na dhambi hiyo kubwa na  isifikie wakati akatafutwa mchawi  wa kulaumiwi”. alisema Balozi Seif.
Balozi Seif amelitaja kundi jengine kubwa la Vijana ambalo chama cha Siasa kinapaswa kuwa na Sera na mfumo  bora utakaowavutia Vijana wengi ili kujitengenezea mazingira mazuri ya kushinda uchaguzi na huo ndio mtazamo wa Chama cha Mapinduzi.
Amesema  Chama kinategemea kazi hiyo ya kuwavutia Vijana kujiunga kwa wingi itasimamiwa na kufanywa na Vijana hao wa CCM wa Vyuo Vikuu ambao changamoto inayowakabili kwa sasa  ni kutoa mbinu ili malengo yaliyokusudiwa yafikiwe mapema iwezekanavyo.
Amewashauri Vijana hao wa Vyuo Vikuu kujidhatiti zaidi katika ujenzi wa Chama chao kama walivyofanya Vijana Wasomi wa Chama cha zamani cha ASP wa Young African Social Union {YASU} waliokuwa wakiwakusanya vijana na  kuwapatia  elimu nyakati za jioni.
Balozi Seif amefahamisha kuwa  kundi la Vijana wa  Afro Shirazy Party {Yasu} lilikuwa na mipango mizuri ya kujenga Chama chao na kupelekea kuanzisha Magazeti ya Kipanga na Tai pamoja na kujenga Jumba la ghorofa maarufu Yasu liliopo Mtaa wa Miembeni Mjini Zanzibar.
Akizungumzia uimara wa Chama cha Mapinduzi katika kipindi cha miaka 39 iliyopita tokea kilipoasisiwa mwaka 1977 Balozi Seif amesema zipo faida nyingi zilizoimarika kupitia CCM ikiwemo uimarishaji wa Muungano, Uongozi wa pamoja , Uchumi pamoja na Demokrasia.
Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM amefahamisha kuwa historia ya Demokrasia Nchini Tanzania  ikiandikwa haitokamilika  bila ya kutoa nafasi ya pekee  kwa CCM kutokana na juhudi zake za kufungua milango ya Demokrasia Nchini.
Balozi Seif alisema Demokrasia madhubuti ndani ya CCM ndio iliyoanzisha Mjadala wa haja ya kuwa na mfumo wa vyama vingi vya Kisiasa na kupelekea kufunguliwa milango ya Demokrasia mwaka 1992.
Ameeleza kwamba ufunguzi huo wa milango ya Demokrasia Nchini chini ya Chama cha Mapinduzi umewezesha kuibuka kwa zaidi ya vyama 18 vya siasa Nchini Tanzania na kupata usajili wa kudumu kutoka msajili wa vyama vya Siasa Tanzania.
Kuhusu hali ya amani inayoendelea kuwepo Nchini Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya CCM Taifa amesema kwa vile Amani ni itikadi iliyoota mizizi ndani ya Chama cha Mapinduzi  kila mfuasi wa chama hicho anatakiwa kuikumbatia kwa mahaba yake yote itikadi hiyo muhimu kwani bila ya hali hiyo Taifa halitaweza kuleta Maendeleo.
Akitoa Taarifa Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyuo Vikuu Tanzania Hamid Saleh Muhina amesema shirikisho hilo limeundwa kwa lengo la  kuwaandaa Vijana katika mazingira ya kisasa ya sayansi na Teknoloji ili wawe  viongozi bora wa hapo baadaye.
Amesema mpango huo ndio njia pekee itakayoliwezesha Taifa kuwa na hazina kubwa ya vijana wasomi watakaokuwa na uwezo wa kutekeleza majukumu yao katika mfumo wa mtandao wa mawasiliano ya kisasa.
Akielezea suala la kufutwa kwa uchaguzi Mkuu Mwenyekiti huyo wa Shirikisho la Vyuo Vikuu Nchini Tanzania  amevitaka vyama vya siasa ambavyo bado havijaamua kushiriki uchaguzi wa marejeo kutafakari kwa makini maamuzi yao ili wananchama wao wasipoteze haki yao ya Kidemokrasia ya kuchagua Viongozi wanaowataka.
Washiriki hao wa Kongamano la maadhimisho ya kutimia miaka 39 ya Chama cha Mapinduzi wameuhakikishia Uongozi wa Juu wa Chama hicho kuwa mbali ya kusimamia uchaguzi wa marejeo ifikapo Tarehe 20 Mwezi wa Machi pia watashiriki vyema kupiga kura kwenye uchaguzi huo ili kukamilisha haki yao ya Kidemokrasi.






Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

4/2/2016.

0 comments:

Post a Comment