Tanzania imetangazwa rasmi kuwa ni mojwapo ya nchi
isiyokuwa na ugonjwa wa polio katika nchi za Afrika katika mkutano wa Tume ya
Afrika ya kuthibitishwa kutokomezwa kwa polio(Afrika Regional
Certification Commission for Polio Eradication).
Kutangazwa kulifanyika katika mkutano huo uliofanyika nchini
Madagascar, Novemba 26, mwaka huu.
Kauli hiyo ilitolewa leo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na
Ustawi wa Jamii, Dkt. Donan Mmbando wakati wa mkutano wake na waandishi wa
habari kuhusu ugonjwa huo ulifanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa wizara hiyo
jijini Dar es Salaam.
“Hii inamaanisha kuwa kwa sasa
hatuna ugonjwa wa polio tena nchini kwa sababu tumeweza kuwafikia watoto wengi
zaidi kwa kuwapatia chanjo ya polio na hivyo kuongeza kinga kwenye
jamii.Kutokana na mafanikio hayo, tunatakiwa bado kuendelea na kutoa chanjo ya
polio kwa watoto wote stahiki ili kuongeza kinga kwa jamii pamoja kuimarisha
mfumo wa ufutiliaji wa mgonjwa yoyote mwenye ulemavu wa ghafla,” alisema Dkt.
Mmbando.
Katibu Mkuu huyo alifafanua kwamba mgonjwa wa mwisho wa polio
alipatikana Julai mwaka 1996 hapa nchini.
Aliongeza kuwa ufuatiliaji wa magonjwa yanayokingwa na chanjo
uliimarishwa na kufikia viwango vinavyo kukubalika kimataifa na kuthibitisha
kuwa watoto wenye umri chini ya miaka 15 waliopata ulemavu wa ghafla
wanapatikana na sampuli zao kuchukuliwa mara moja.
Hivyo kuanzia mwaka 1997 mpaka Oktoba 2015 jumla
ya sampuli 6,249 za watoto waliopata ulemavu zilipelekwa kwenye maabara za
kimataifa na kuthibitishwa kuwa hakuna sampuli iliyoonesha uwepo wa
ugonjwa wa polio.
Dkt. Mmbando aliongeza kwamba wizara yake kupitia Mpango wa Taifa
wa Chanjo imekuwa ikihakikisha kwamba watoto wote Tanzania wanapata chanjo
zenye ubora ili kuwakinga dhidi ya magonjwa ya milipuko ikiwemo ugonjwa wa
polio.
“ Mwitikio wa wananchi kwa huduma za chanjo umeendelea kuwa mkubwa
kwa takribani miaka kumi iliyopita na kufikia viwango vya zaidi ya
asilimia 90 kwa kila chanjo kitaifa na wilaya zaidi ya asilimia 80 kufanya
vizuri katika kutoa huduma za chanjo,” alisema Dkt. Mmbando.
Ugonjwa wa polio ni ugonjwa wa kuambukizwa unaosababishwa na virusi
vya polio, unaathiri misuli na mfumo wa fahamu hivyo
kusababisha kupooza kwa viungo hasa na miguu na wakati mwingine
kusababisha hata kifo .
Alisema ulemavu huo ukishajitokeza huwa ni wa kudumu, waathirika
wakuu wa ugonjwa huo ni watoto hasa waliaochini ya umri wa miaka mitano.
Aliongeza kwamba ugonjwa huo unazuilika kwa chanjo ya
polio ambayo ni salama na inatolewa bure na Serikali katika vituo
vyote vya huduma ya afya.
Dkt. Mmbando alitoa pongezi kwa wananchi wote wakiwemo viongozi na
watendaji wa ngazi zote kwa ushirikiano wao ambao umeifikisha Tanzania kwenye
ramani ya dunia ya kutokuwa na ugonjwa huo.
Aidha wizara imewashukuru wajumbe wa kamati mbalimbali za
kutokomeza ugonjwa huo chini ya uongozi wa Profesa Ester Mwaikambo, watendaji
wa Mpango wa Taifa wa Chanjo na wadau wa chanjo, wadau wa mfuko wa pamoja wa
Pamoja wa Afya , WHO, GAVI, UNICEF, CHAI, USAID ,REDCROSS NA LIONS CLUB kwa
kazi kubwa ya kuhakikisha kila mtoto mlengwa anapata chanjo.
Tanzania ni miongoni mwa nchi nne ambazo zimepata cheti hicho
mwaka huu, katika bara hilo.Pia ni nchi ya 33 kati ya nchi 47 za
bara hilo ziliowahi kupata cheti hicho.
Katika bara hilo bado nchi 14 ambazo hazijawahi kupata cheti
hicho.
0 comments:
Post a Comment