December 02, 2015

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kitampa ushirikiano Rais Dk. John Magufuli ili kutimiza kwa ufanisi zaidi mapambano yake dhidi ya mafisadi na mikakati mingine ya kuinua uchumi wa Watanzania.

Kimesema aliyoanza kuyafanya na atakayoyafanya baadaye katika uongozi wake wa Urais anatekeleza yale yaliyomo katika ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2015-2020.

Hayo yalisemwa na Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye alipokuwa akijibu maswali kadhaa yaliyoulizwa na baadhi ya wahariri aliokuwa akizungumza nao  katika ziara aliyofanya leo katika Kampuni ya New Habari Corporation, Sinza jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya wahariri walihoji ni kwa nini CCM haijitokezi kumpongeza Dk. Magufuli katika juhudi ambazo ameanza kuonyesha katika kupambana na ufisadi ikiwemo kubana fedha za walipa kodi ambazo zingepotea bure katika masuala yasiyo ya lazima na wakati huohuo kuanza kuwabana wafanyabiashara wanaodaiwa kukwepa kulipa ushuru.

"Yapo mengi tuliyoainisha katika ilani yetu ya Uchaguzi, na yote yanahusiana sana na haya mnayoyaona yanafanywa na Rais Dk. John Magufuli, tena Ilani hii tumeitunga hata kabla ya kumteua kugombea Urais, Sasa anachofaya ni kuitekeleza ilani hii, isipokuwa mbinu anazotumia ni ubunifu wake na hili hatuna tatizo nalo kama Chama maana kiongozi wa aina hii ndiye tuliyemtaka", alisema Nape.

"Najua wapo wanaojaribu kutengeneza mazingira ya kutaka kumtenganisha Dk. Magufuli na CCM, nawaambieni Dk. Magufuli ni zao la CCM, hivyo ni upotoshaji wa hali ya juu kujaribu kuuaminisha umma kwamba anayofanya Dk. Magufuli hayana uhusiano na maelekezo ya CCM", aliongeza Nape.

Alisema, baada ya kutengeneza ilani yake, CCM ilidhamiria kwamba, awamu hii ya tano ni ya kutafsiri uchumi katika nyanja za huduma za Jamii, ikiwemo miundomboni, maji, afya na elimu.

"Ni kutokana na lengo hili, ndiyo sababu tukakaa kwa makini na kuhakikisha ilani hii ya sasa tunamkabidhi mwana CCM ambaye utekelezaji wake hautakuwa wa mashaka mashaka, Ndiyo huyo Dk. Magufuli .Bila shaka sasa na ninyi ni mashahidi mmeanza kuuona utekelezaji wake wa ilani", alisema Nape.

Akizungumzia kuhusu Rais Dk. Magufuli kuchelewa kutangaza Baraza lake la Mawaziri, Nape alisema, Chama Cha Mapinduzi kimeshaunda serikali kwa kumpata Rais, kilichobaki sasa ni kwa Rais mwenyewe kuteua watendaji wake lakini katika kufanya hivyo hakuna muda aliopangiwa kuanza kufanya hivyo na hashurutishwi na Chama wala sheria.

Nape alisema, Dk. Magufuli hachelewi kuteua Baraza la Mawaziri kwa sababu anakosa wakuwateua, isipokuwa, anayo namna na muda ambao mwenyewe Kama Rais amejipangia, na mda huo ukijiri wa kuamua kufanya hivyo atafanya.

"Tatizo hapa ni kwamba mnayo kiu kubwa ya kutaka kujua nani atawateua, sasa kiu yenu imepita kiasi, ndiyo maana mnaanza kuhoji, lakini mimi naamini Dk. Rais Magufuli ataikata kiu yetu wala msipate taabu ya kuhoji kila kukicha", alisema Nape.

Nape alisema, mbali na Chama kutengeneza ilani ambayo italeta mageuzi makubwa ya kiuchumi hapa nchini, pia Watanzania watarajie kuona mageuzi makubwa ndani ya CCM, kwa sababu yapo njiani kuwadia.

"Kama ilivyo kawaida yetu, kila baada ya uchaguzi mkuu huwa tunafanya tathmini, baada ya tathmini hiyo huwa lazima tufanye mageuzi kwa yale ambayo tumebaini kuwa ni kikwazo kwa uhai na maendeleo ya Chama katika nyanja mbalimbali na mageuzi haya tunayafanya kuzingatia mahitaji ya sasa na wakati ujao", alisema Nape.

Kuhusu Mwenyekiti wa sasa Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete kumwachia Ueneyekiti Rais Dk. Magufuli, Nape alisema hayo si mambo mageni kwa  CCM. Imekuwa ikifanyika katika awamu zote za Urais, hivyo Kikwete anaweza akaamua kumwachia kabla ya uchaguzi mkuu wa CCM utakaofanyika mwaka 2017 au kabla ya hapo akiona inafaa.

Zanzibar
Akizungumzia mgogoro wa Zanzibar uliotokana na kufutwa uchaguzi mkuu wa Rais wa Zanzibar, Nape alikiri kamba ni mbaya na unaitia doa Tanzania lakini akasisitiza kwamba njia pekee ya kuumaliza ni kwa mazungumzo baina ya viongozi wa ndani bila kushirikisha mataifa ya nje.

Alisema, msingi wa mgogoro uliojitokeza Zanzibar, si wa kisheria bali ni wa kisiasa zaidi, hivyo juhudi ziwekwe kwenye mazungumzo kuutatua na baada ya kuutatua yaendelee kufanyika mazungumzo ambayo yataleta suluhisho la kudumu kwa kuwa imekuwa ni kawaida kwa Zanzibar kuzuka migogoro kila baada ya uchaguzi mkuu jambo linaloonyesha kuwa tatizo ni la asili zaidi kuliko inavyodhaniwa.

Katika mazungumzo yake na wahariri hao wa New Habari Corporation Ltd, Wachapishaji wa magazeti ya Raia, Mtanzania na Dimba, alivitaka vyombo vya habari nchini, sasa kushirikiana na Serikali kulijenga taifa.

"Tunajua wakati wa kampeni kulikuwa na mambo mbalimbali ambayo wakati mwingine vyombo vya habari vililazimika kukampenia vinaowaona kuwa wanafaa kutokana na sababu mbalimbali, lakini kama tulivyokuwa tukisema, kwamba baada ya uchaguzi maisha yataendelea, sasa umefika wakati wa kuendelea na maisha tuwe kitu kimoja", alisema Nape.

Alivitaka vyombo vya habari, kusaidia kuishauri Serikali na CCM  katika kutekeleza yaliyo bora kwa taifa na hata pale vyombo hivyo vitakapoona kwamba Chama au serikali vinaenda kinyume, visihofu kukosoa.

Kwa upande wao, Mhariri Mtendaji wa Habari Corporation, Absalom Kibanda alimpongeza Nape kwa ushirikiano ambao amekuwa akivipa vyombo vya habari na kumtaka aendelee kuacha milango wazi kwa waandishi wa habari kama ambavyo amekuwa akifanya.

Ziara hiyo ya Nape aliyoianza jana kwenye vyombo vya habari inatarajiwa kuendelea kesho kwa kutembelea vyombo vingine vya habari vyenye makao yake makuu jijini Dar es Salaam.



Mpekuzi

0 comments:

Post a Comment