Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kitampa ushirikiano Rais Dk.
John Magufuli ili kutimiza kwa ufanisi zaidi mapambano yake dhidi ya mafisadi
na mikakati mingine ya kuinua uchumi wa Watanzania.
Kimesema aliyoanza kuyafanya na atakayoyafanya baadaye katika
uongozi wake wa Urais anatekeleza yale yaliyomo katika ilani ya Uchaguzi ya CCM
ya 2015-2020.
Hayo yalisemwa na Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye
alipokuwa akijibu maswali kadhaa yaliyoulizwa na baadhi ya wahariri aliokuwa
akizungumza nao katika ziara
aliyofanya leo katika Kampuni ya New Habari Corporation, Sinza jijini Dar es
Salaam.
Baadhi ya wahariri walihoji ni kwa nini CCM haijitokezi
kumpongeza Dk. Magufuli katika juhudi ambazo ameanza kuonyesha katika kupambana
na ufisadi ikiwemo kubana fedha za walipa kodi ambazo zingepotea bure katika
masuala yasiyo ya lazima na wakati huohuo kuanza kuwabana wafanyabiashara
wanaodaiwa kukwepa kulipa ushuru.
"Yapo mengi tuliyoainisha katika ilani yetu ya Uchaguzi, na
yote yanahusiana sana na haya mnayoyaona yanafanywa na Rais Dk. John Magufuli,
tena Ilani hii tumeitunga hata kabla ya kumteua kugombea Urais, Sasa anachofaya
ni kuitekeleza ilani hii, isipokuwa mbinu anazotumia ni ubunifu wake na hili
hatuna tatizo nalo kama Chama maana kiongozi wa aina hii ndiye
tuliyemtaka", alisema Nape.
"Najua wapo wanaojaribu kutengeneza mazingira ya kutaka
kumtenganisha Dk. Magufuli na CCM, nawaambieni Dk. Magufuli ni zao la CCM,
hivyo ni upotoshaji wa hali ya juu kujaribu kuuaminisha umma kwamba anayofanya
Dk. Magufuli hayana uhusiano na maelekezo ya CCM", aliongeza Nape.
Alisema, baada ya kutengeneza ilani yake, CCM ilidhamiria kwamba, awamu hii ya tano ni
ya kutafsiri uchumi katika nyanja za huduma za Jamii, ikiwemo miundomboni,
maji, afya na elimu.
"Ni kutokana na lengo hili, ndiyo sababu tukakaa kwa makini
na kuhakikisha ilani hii ya sasa tunamkabidhi mwana CCM ambaye utekelezaji wake
hautakuwa wa mashaka mashaka, Ndiyo huyo Dk. Magufuli .Bila shaka sasa na ninyi ni mashahidi mmeanza
kuuona utekelezaji wake wa ilani", alisema Nape.
Akizungumzia kuhusu Rais Dk. Magufuli kuchelewa kutangaza Baraza
lake la Mawaziri, Nape alisema, Chama Cha Mapinduzi kimeshaunda serikali kwa
kumpata Rais, kilichobaki sasa ni kwa Rais mwenyewe kuteua watendaji wake
lakini katika kufanya hivyo hakuna muda aliopangiwa kuanza kufanya hivyo na
hashurutishwi na Chama wala sheria.
Nape alisema, Dk. Magufuli hachelewi kuteua Baraza la Mawaziri
kwa sababu anakosa wakuwateua, isipokuwa, anayo namna na muda ambao mwenyewe
Kama Rais amejipangia, na mda huo ukijiri wa kuamua kufanya hivyo atafanya.
"Tatizo hapa ni kwamba mnayo kiu kubwa ya kutaka kujua nani
atawateua, sasa kiu yenu imepita kiasi, ndiyo maana mnaanza kuhoji, lakini mimi
naamini Dk. Rais Magufuli ataikata kiu yetu wala msipate taabu ya kuhoji kila
kukicha", alisema Nape.
Nape alisema, mbali na Chama kutengeneza ilani ambayo italeta
mageuzi makubwa ya kiuchumi hapa nchini, pia Watanzania watarajie kuona mageuzi
makubwa ndani ya CCM, kwa sababu yapo njiani kuwadia.
"Kama ilivyo kawaida yetu, kila baada ya uchaguzi mkuu huwa
tunafanya tathmini, baada ya tathmini hiyo huwa lazima tufanye mageuzi kwa yale
ambayo tumebaini kuwa ni kikwazo kwa uhai na maendeleo ya Chama katika nyanja
mbalimbali na mageuzi haya tunayafanya kuzingatia mahitaji ya sasa na wakati
ujao", alisema Nape.
Kuhusu Mwenyekiti wa sasa Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete kumwachia
Ueneyekiti Rais Dk. Magufuli, Nape alisema hayo si mambo mageni kwa CCM.
Imekuwa ikifanyika katika awamu zote za Urais, hivyo Kikwete anaweza akaamua
kumwachia kabla ya uchaguzi mkuu wa CCM utakaofanyika mwaka 2017 au kabla ya
hapo akiona inafaa.
Zanzibar
Akizungumzia mgogoro wa Zanzibar uliotokana na kufutwa uchaguzi
mkuu wa Rais wa Zanzibar, Nape alikiri kamba ni mbaya na unaitia doa Tanzania
lakini akasisitiza kwamba njia pekee ya kuumaliza ni kwa mazungumzo baina ya viongozi wa ndani bila kushirikisha
mataifa ya nje.
Alisema, msingi wa mgogoro uliojitokeza Zanzibar, si wa kisheria
bali ni wa kisiasa zaidi, hivyo juhudi ziwekwe kwenye mazungumzo kuutatua na
baada ya kuutatua yaendelee kufanyika mazungumzo ambayo yataleta suluhisho la
kudumu kwa kuwa imekuwa ni kawaida kwa Zanzibar kuzuka migogoro kila baada ya
uchaguzi mkuu jambo linaloonyesha kuwa tatizo ni la asili zaidi kuliko
inavyodhaniwa.
Katika mazungumzo yake na wahariri hao wa New Habari Corporation
Ltd, Wachapishaji wa magazeti ya Raia, Mtanzania na Dimba, alivitaka vyombo vya
habari nchini, sasa kushirikiana na Serikali kulijenga taifa.
"Tunajua wakati wa kampeni kulikuwa na mambo mbalimbali
ambayo wakati mwingine vyombo vya habari vililazimika kukampenia vinaowaona
kuwa wanafaa kutokana na sababu mbalimbali, lakini kama tulivyokuwa tukisema,
kwamba baada ya uchaguzi maisha yataendelea, sasa umefika wakati wa kuendelea
na maisha tuwe kitu kimoja", alisema Nape.
Alivitaka vyombo vya habari, kusaidia kuishauri Serikali na
CCM katika kutekeleza
yaliyo bora kwa taifa na hata pale vyombo hivyo vitakapoona kwamba Chama au
serikali vinaenda kinyume, visihofu kukosoa.
Kwa upande wao, Mhariri Mtendaji wa Habari Corporation, Absalom
Kibanda alimpongeza Nape kwa ushirikiano ambao amekuwa akivipa vyombo vya
habari na kumtaka aendelee kuacha milango wazi kwa waandishi wa habari kama
ambavyo amekuwa akifanya.
Ziara hiyo ya Nape aliyoianza jana kwenye vyombo vya habari
inatarajiwa kuendelea kesho kwa kutembelea vyombo vingine vya habari vyenye
makao yake makuu jijini Dar es Salaam.
Mpekuzi
0 comments:
Post a Comment