December 11, 2015


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi  ameagiza  kufutwa mikataba yote ya makubaliano ya  ukodishwaji wa Nyumba za Serikali zilizojengwa maalum kwa kuwasaidia Wananchi wa kipato cha Chini  unayofanywa kijanja  na  baadhi ya watu  pamoja na Kampuni binafsi.
Alisema tabia hiyo iliyojengeka kwa muda mrefu sasa inatumiwa na wajanja hao wanaokodishwa Nyumba  na Serikali na baadaye kubuni mikataba mipya ya kuwakodisha watu wengine kwa nia ya kupata  faida kubwa zaidi (Maarufu kilemba).
Balozi Seif Ali Iddi ametoa Kauli hiyo alipofanya ziara fupi ya kufuatilia Mikataba ya Wafanyabiashara waliokodishwa  milango ya Maduka katika Jumba la Maendeleo Nambari Kumi  Michenzani Mjini Zanzibar ambayo baadhi ya waliokodishwa milango hiyo na Serikali tayari  wameshaikodisha  kwa  watu wengine.
Amesema tabia ya baadhi ya Watu hao kutumia mali za Serikali walizopewa kwa misingi ya kupunguza ukali wa maisha  na kuwauzia au kuwakodisha watu wengine waelewe kwamba wanafanya dhulma na dhambi kubwa.
Balozi Seif ameupongeza Uongozi wa Shirika la Nyumba Zanzibar (ZHC) kwa uamuzi iliyochukuwa ya kuwafutia mikataba wajeta wake wa mwanzo  iliyowapa milango la Maduka na wakaamua kuikodisha kwa watu wengine.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameonya  kwamba tabia kama hiyo imejengeka pia katika Nyumba zilizowekwa Wakfu na kuishauri Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana Zanzibar kufanya utafiti na kuwabaini wapangaji wake wenye tabia kama hiyo.
Mapema Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Nyumba Zanzibar Moh’d  Hafidh Rajab amesema  Watendaji wa Shirika hilo wameanza ukaguzi Maalum wa kuzipitia Nyumba zote za Serikali zilizokodishwa kwa watu na Taasisi tofauti hapa Nchini.
Hafid amesema ukaguzi huo utatoa fursa kwa Uongozi wa Shirika  hilo kufanya marekebisho ya kodi zilizofungwa katika mikataba ya zamani ili iende na wakati na soko liliopo hivi sasa.
Amesema Shirika la Nyumba la Zanzibar lililoasisiwa hivi karibuni baada ya kupata baraka za Baraza la Wawakilishi Zanzibar linahitajika kujitegemea wenyewe badala ya kusubiri ruzuku inayotolewa na Serikali Kuu.
Akitoa shukrani zake Mmoja wa wamiliki wa Maduka yaliyopo  Michenzani ambae ni Meneja wa Kampuni ya A l – Salam na Seib Ruila Yussuf Juma Msanif  ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Shirika lake la Nyumba kwa uamuzi wake wa kukagua majengo yake mbali mbali.
Yussuf amesema uamuzi huo wa busara na hekima umewapa faraja wao binafsi na Kuliomba Shirika la Nyumba kufikiria upya kodi zake  inazotoza kwa lengo la kuwapa tahfifu Wafanyabiashara wachanga ili kuwa na uwezo mzuri wa kulipa kodi.
Mlango mmoja wa Duka hapo Michenzani ulikuwa ukikodishwa Mteja kutoka Serikalini kwa Shilingi elfu Thamanini kwa Mwaka wakati mkodishwa huyo anaamuwa kukodisha tena kwa Mtu wa Pili wa Dola za Kimarekani  mia 450  kwa mwaka sawa na Shilingi Laki Tisa na Thamanini (980,0000)  za Kitanzania.
Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alikutana na Kamati ya  Taifa ya Sherehe za Maulidi ya kuzaliwa Kiongozi wa Dini ya Kiislamu Mtume Muhammad  { SAW }.
Kamati hiyo aliyokutana nayo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar pamoja na mambo mengine  Mwenyekiti wake Sheikh Sherali Shamsi alimuelezea matayarisho yanayoendelea ya Maulidi hayo yanayofanyika Kitaifa kila mwaka hapa Zanzibar.







Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
11/12/2015.

0 comments:

Post a Comment