November 14, 2015


Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi CUF Maalim Seif Sharif Hamad, amerejea kauli yake ya kutotambua kufutwa kwa uchaguzi mkuu wa Zanzibar uliofanyika tarehe 25 mwezi uliopita.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam mara baada ya kikao cha mashauriano na viongozi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA, Maalim Seif amesema kinachohitajika na kuendelea na mchakato wa kuhakiki kura zilizobakia na mshindi kutangazwa.
Kuhusu tamko lililotolewa na serikali juu ya kufutwa rasmi kwa uchaguzi huo kupitia tangazo lililochapishwa kwenye gazeti rasmi la serikali mapema wiki hii Maalim Seif amesema tamko hilo limekosa uhalali tangu lilipotolewa na Mwenyekiti wa ZEC Bw Jecha Salim Jecha .
Maalim Seif ambaye pia ni Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia CUF amesema Chama chake hakijalizingatia tamko hilo na wala hakijadili uwezekano wa kurejewa kwa uchaguzi huo, kwa madai kuwa uchaguzi ulikamilika bila ya kuwepo malalamiko kutoka chama chochote cha siasa na wala Tume ya Uchaguzi.
Mapema akizungumza baada ya kikao hicho cha mashauriano, aliyekuwa mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chadema Mhe. Edward Lowassa amesema kikao hicho kilichojadili Mkwamo wa kisiasa Zanzibar kimekwenda vizuri.
Hata hivyo amesema ufafanuzi zaidi utatolewa Jumapili ijayo ambapo viongozi hao wanakusudia kuzungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Kabla ya kikao hicho Maalim Seif alifanya mazungumzo na Balozi wa Umoja wa Ulaya (EU) Bw. Filberto Seregondi katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam na kuelezea hatua zinazochukuliwa kukwamua mkwamo wa kisiasa Zanzibar.
Balozi Seregondi ambaye anamaliza muda wake wa utumishi hapa nchini, aliambatana na ujumbe wa waangalizi wa uchaguzi mkuu wa Tanzania kutoka Umoja huo.
Hassan Hamad, OMKR

0 comments:

Post a Comment