May 08, 2014

 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                                                 8 Mei , 2014
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema Sheria Namba 2 ya Utumushi wa Umma ndio sheria mama za utumishi hivyo Taasisi na Wakala wa Serikali hazina budi kuzingatia sheria hiyo katika masuala yote yanayohusu watumishi wake.
 Amesema kuwa pamoja na kuwa taasisi na wakala wa Serikali kuwa ni vyombo vilivyopewa mamlaka kujiendesha lakini bado vinabaki kuwa vya serikali hivyo sheria ama kanuni za utumishi za taasisi hizo hazina budi kwenda sambamba na Sheria hiyo.
 Alifafanua kuwa mashirika na wakala wa serikali wanatekeleza majukumu ya serikali ambayo Serikali yenyewe kwa sababu mbalimbali imeamua au haiwezi kuzitekeleza kwa ufanisi au uhuru unaotakiwa.
 Akizungumza katika mkutano uliojumushia wenyeviti wa Bodi za Taasisi, mashirika na wakala wa serikali pamoja na wajumbe wa bodi hizo Dk. Shein alisema lengo la kupitisha sheria hiyo ni kuhakikisha kuwa utumishi Serikalini unakuwa bora na imara ili kuweza kutoa huduma stahiki kwa wananchi.
 Alibainisha pamoja na awamu zote za Serikali zilizopita kufanya jitihada na kuchukua hatua mbalimbali kuimarisha utumishi serikalini lakini uzoefu unaonesha kuwa bado kuna udhaifu kwenye utumishi wa umma katika kutekeleza majukumu ya serikali.
 “Tumekuwa tukifanya mageuzi kuimarisha mazingira ya kazi kwa kuongeza nyenzo za kisasa na kuongeza maslahi ya watumishi lakini tumeshindwa kufikia viwango tunavyo tarajia“ alieleza Dk. Shein.
 Alifafanua kuwa udhaifu huo unatokana na usimamizi usioridhisha wa Sheria ya Utumishi wa Umma pamoja na kanuni zake hivyo kuwafanya watumishi wengi kutozingatia nidhamu na kutotimiza wajibu wao wawapo kazini matokeo yake ni kuzorotesha utendaji katika Serikali na taasisi zake.
 “Sheria zipo na kanuni zipo lakini mambo hayaendi hivyo Serikali ya Awamu hii iliamua kuiweka Sheria Namba 2 ya Utumushi wa Umma iliyopitishwa mwaka 2011 katika Katiba ili suala la utumishi wa umma lipate msukumo wa kisheria na kutoa matunda yanayotarajiwa” Dk. Shein alifafanua.
 Kwa hiyo alitoa wito kwa wizara, taasisi, mashirika na wakala wa serikali kuzingatia Katiba, Sera na Sheria ya Utumushi wa Umma huku akitaka Kamisheni ya Utumishi wa Umma ambayo imeanzishwa kwa mujibu wa sheria hiyo kupewa ushirikiano stahiki ili iweze kutekeleza majukumu yake.
 Dk. Shein alibainisha kuwa Kamisheni ya Utumishi wa Umma ambacho ndicho chombo cha juu katika masuala ya utumishi wa umma imekuwa ikikutana na vikwazo mbalimbali katika kutekeleza wajibu wake na kuwataka viongozi na watendaji kutokiogopa chombo hicho kwani kiko kwa maslahi ya nchi.
 “Tuipe ushirikiano Kamisheni, haikuja kuchukua wala kuingilia madaraka ya mtu bali kutekeleza matakwa ya kisheria ambayo kila taasisi na kiongozi wake anapaswa kuyatekeleza” Dk. Shein alisisitiza.
 Kuhusu uhusiano kati ya bodi za taasisi za serikali na wizara, Mhe Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliwaambia washiriki wa mkutano huo ambao ulijumuisha pia mawaziri na makatibu wakuu kuwa ni wa lazima kwa kuwa wajibu wa Bodi ni kuishauri wizara.
 “Lazima kuwepo mawasiliano ya karibu kati ya Bodi na Wizara na kama kumetokea tofauti mazungumzo yafanyike kumaliza tofauti hizo kwa faida ya nchi” Mhe Rais alisisitiza.
 Mapema akitoa mada kuhusu Uhusiano baina ya Utumishi wa Umma na Mashirika ya Serikali na Taasisi zinazojitegemea Mwanasheria Mkuu wa Serikali Othman Masoud alieleza kuwa uhuru wa mashirika hayo ni wa kuyawezesha tu kuleta ufanisi lakini yanapaswa kuzingatia nguzo kuu za serikali.
 Alifafanua kuwa uwajibikaji wa Serikali ni pamoja na mashirika na taasisi zake hivyo mashirika na taasisi hizo zinatekeleza majukumu ya serikali na kuongeza kuwa Katiba inabainisha kuwa watumishi wote wa taasisi hizo ni watumishi wa serikali.
 Kwa upande wake Katibu Mkuu Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee katika mada yake ya Uongozi, Uwajibikaji, na Umuhimu wa Maadili katika Taasisi za Serikali  alitiliza mkazo juu ya viongozi na watendaji wakuu kuwa mfano katika utendaji na kujenga utamaduni utakaopelekea kuleta ufanisi katika taasisi wanazoziongoza.  
 

0 comments:

Post a Comment