February 03, 2016

Wafuasi wa Chama Cha Wananchi CUF, wameunga mkono tamko lililotolewa na Baraza Kuu la Uongozi la Chama hicho la kutoshiriki uchaguzi wa marudio uliopangwa kufanyika tarehe 20/03/2016 Visiwani Zanzibar.
Wanachama hao kupitia viongozi wao wa Wilaya na Majimbo ya Unguja, wameunga mkono tamko hilo baada ya kupata maelezo kutoka kwa  Katibu Mkuu wa chama hicho Maalim Seif Sharif Hamad, kwenye mkutano maalum uliofanyika ukumbi wa Majid Kiembe Samaki Zanzibar.
Wamesema hakuna sababu ya kushiriki uchaguzi huo ambao wamesema ni wa kulazimisha na hauwezi kuwa huru na wa haki.
Wameeleza kuwa uchaguzi halali, huru na wa haki ulishafanyika Oktoba 25, 2015 na wananchi wengi walimchagua mgombea wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad lakini ulifutwa bila ya kuwepo sababu za msingi.
Mapema akizungumza na viongozi hao wa CUF ngazi ya Wilaya na Majimbo kwa upande wa Unguja, Maalim Seif amesema Chama hicho hakitorudi nyuma katika kutetea maamuzi ya Wazanzibari waliyoyafanya tarehe 25 Oktoba 2015.
Amesema licha ya Chama hicho kutangaza kutoshiriki uchaguzi huo wa marudio, juhudi mbali mbali zinaendelea kufanywa kuhakikisha kuwa Chama Cha Mapinduzi CCM kinaondoka madarakani.
Akizungumzia hali ya kisiasa Zanzibar Maalim Seif amesema siasa za nguvu na kimabavu zinazoendeshwa na Chama Cha Mapinduzi hazitoisaidia Zanzibar na badala yake zinaweza kuzidisha mgogoro uliopo.
Maalim Seif ameishutumu Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuingilia uchaguzi wa Zanzibar na kupelekea kuwepo kwa mgogoro mkubwa wa kisiasa na kikatiba.
Maalim Seif pia amewashutumu baadhi ya viongozi wakiwemo wa dini wanaojaribu kupotosha ukweli na kuunga mkono uamuzi batili wa kurejewa uchaguzi uliotangazwa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar.

Akizungumzia kuhusu vikao vya kutafuta muafaka wa mkwamo wa kisiasa vilivyokuwa vikifanyika Ikulu ya Zanzibar, Maalim Seif amesema katika vikao hivyo walijadiliana na kukubaliana kuwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar imepoteza sifa ya kusimamia uchaguzi, lakini ameshangazwa na kitendo cha Tume hiyo hiyo kutangaza uchaguzi wa marejeo, huku viongozi wa CCM walioshiriki mazungumzo hayo wakiunga mkono.

Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa CUF Ismali Jussa Ladhu,
akizungumza na viongozi hao wa Wilaya na Majimbo ya Unguja

Baadhi ya viongozi wa Wilaya na Majimbo wa CUF upande wa Unguja,
wakijitokeza kumsikiliza Katibu Mkuu wa Chama hicho
Maalim Seif Sharif Hamad, huko ukumbi wa Majid Kiembe Samaki.

0 comments:

Post a Comment