February 03, 2016

Vijana wametakiwa kujitambua na kuacha kuchezewa kiakili  kunakosababisha  kujiingiza katika wimbi la matatizo ya kimaisha.
Mkurugenzi na muasisi wa Jumuiya ya kuelimisha jamii katika masuala ya maendeleo na ustawi wa Jamii Zanzibar {Wide} Bi Rehema Mwinyi amesema kutokana na mabadiliko ya mfumo wa kimaisha uliopo sasa kundi hilo hasa wale wanaopata elimu wanapaswa kutumia taaluma yao katika kutafuta maisha kupitia mfumo wa ujasiri amali badala ya kusubiri ajira chache zilizopo Serikalini.
Bibi Rehema Mwinyi ameeleza hayo alipokuwa akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipofika kujitambulisha rasmi Ofisini Vuga Mjini Zanzibar akiuongozana Ujumbe wa Viongozi Watatu wa Jumuiya hiyo.
Amesema mradi wa kuleta shukrani kwa jamii kufuatia wanajumuiya hiyo kufaidika na misaada ya Serikali katika kuwaandaa  Kitaaluma umelenga kuyajengea uwezo wa kiujasiri amali makundi ya Wanawake na Vijana hapa Zanzibar.
Amesema wapo Vijana na akina mama wengi mitaani waliobarikiwa kuwa na vipaji vya kujiendesha kimaisha lakini wanashindwa kuvitumia ipasavyo kutokana na ufinyu wa Taaluma pamoja na mitaji ya kuanzia miradi wanayoamua kuianzisha.
Mkurugenzi huyo wa Wide Zanzibar Bibi Rehema ameeleza kwamba mradi huo umelenga kuanzisha matamasha kwa ajili ya kuibua vipaji hivyo katika Nyanja mbali mbali ili kuwatengeneza kwa faida yao ya baadae.
Naye Mshauri wa Jumuiya ya Wide Zanzibar Bwana Said Alawi alisema ipo mipango ya muda mrefu ya Jumuiya hiyo katika kutoa elimu ya kuliendeleza bonde la Uwanja wa Farasi liliopo Kwahani Mjini Zanzibar
lengo likiwa ni kulirejeshea hadhi yake ya asili ya kuwa sehemu za Burdani na si kuwa eneo hatarishi.
“ Eneo hilo lilipata umaarufu wa kuitwa uwanja wa Farasi kutokana na watu wengi kulitumia kwa burdani ya michezo ya Farasi miaka mingi iliyopita ”. amesema.
Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amesema Jumuiya ya Wide inapaswa kuendelea kuwaongoza Vijana njia yenye muelekeo sahihi wa maisha yao.
Akigusia suala la mazingira ambalo limo ndani ya mpango kazi wa Jumuiya hiyo Balozi Seif  amesema mazingira yaliyopo nchini hivi sasa yamechafuka katika maeneo mengi kutokana na usimamizi mbovu wa watendaji wa Halmashauri za Wilaya pamoja na Serikali za Mitaa.

Alisema ipo tabia ya baadhi ya watu kutafuta nafasi ndogo zilizomo ndani ya mitaa na kuzitumia katika kuanzisha miradi inayochafua mazingira  na hatimae kusumbua jamii.

0 comments:

Post a Comment