February 15, 2016

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amesema kwa vile Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar imeshatangaza Tarehe ya Kurejewa kwa Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar  yeye binafsi haoni umuhimu wa kurejewa kwa mazungumzo kati ya Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad na Rais wa Zanzibar Dr. Ali Mohammed Shein .
Amesema mazungumzo hayo kwa sasa hayana tija yoyote kwa vile Wananchi katika kipindi hichi wameanza kujiweka tayari wakijiandaa kupiga kura kufuatia  Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar { ZEC} kufuta matokeo ya uchaguzi Tarehe 28 Oktoba mwaka 2015.
Akizungumza na Waandishi wa Habari kwenye Uwanja wa ndege wa Pemba akijiandaa kurejea Kisiwani Unguja baada ya kumaliza ziara yake ya siku Tatu Kisiwani Pemba kukagua shughuli mbali mbali za Maendeleo akiwa Mtendaji Mkuu wa Serikali Balozi Seif Ali Iddi amesema iwapo yapo malalamiko yoyote muhusika wake ana wajibu wa kwenda Mahakamani kwa hivi sasa.
Balozi Seif amesema mazungumzo ya pamoja kati ya Rais wa Zanzibar na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi {CUF } Maalim Seif Sharif Hamad  kuhusu kufutwa kwa Uchaguzi Mkuu yalifanyika kwa maombi ya Maalim Seif ambae yeye binafsi ndie aliyeamua kujiondoa kwenye maendeleo ya vikao vya mazungumzo hayo.
Amesema kinacholikabili Taifa kwa wakati huu ni suala la marejeo ya uchaguzi na kuwaomba watu walioamua kutoshiriki uchaguzi huo wa marudio ni vyema wakabakia nyumbani ili kutoa fursa kwa wenzao waliokubali kushiriki watumie haki yao ya Kidemokrasia kuwachaguwa Viongozi wanaowataka.
Balozi Seif amefahamisha kwamba hata yeye anaheshimu maamuzi ya Tume ya Uchaguzi  ya Z anzibar ambayo haiwezi kuingiliwa na chombo chochote licha ya kwamba tayari alikuwa ameshashinda na kupewa cheti kinachothibitisha kuwa Mwakilishi wa Jimbo la Mahonda.
“Tupo tuliokwishashinda kwenye chaguzi zetu za Majimbo na kupewa vyeti vinavyothibisha ushindi huo lakini baadhi yetu kwa nini tuendelee kushutumu maamuzi ya tume ambayo kutokana na sababu za msingi ilizoeleza  za kujitokeza kwa dosari kadhaa kwenye zoezi zima ikalazimika kufuta matokeo na uchaguzi wote ? ”. ameuliza Balozi Seif.
Akizungumzia uvumi uliojitokeza  wa kuwepo kikundi cha Vijana wanaopiga watu katika badhi ya maeneo maarufu Mazombi Balozi Seif amesema hana taarifa yoyote iliyomfikia akiwa kama Kiongozi wa Juu wa Serikali kuhusu shutma hizo.
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ametoa agizo kwa vyombo 
vya Ulinzi kufanya uchunguzi dhidi ya shutuma hizo na pale itakapobainika kuwepo kwa shutma hizo vifanye juhudi ya kuwakamata wahusika hao na kuwafikisha mbele ya Dola ili sheria ichukuwe mkondo wake.
Balozi Seif ameeleza kwamba nia ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Ile ya Jamuhuri ya Mauungano wa Tanzania ni kuiona nchi inaendelea  kubakia katika hali ya amani na utulivu wakati wote kabla na baada ya uchaguzi.
Amewaasa na kuwaomba Wananchi wa maeneo mbali mbali Kisiwani Pemba kuendelea kuishi kwa amani na upendo na kushirikiana katika mambo yao bila ya kuendekeza zaidi itikadi zao za Kisiasa ambazo tayari zimeshaonyesha muelekeo mbaya.

Ameeleza kwamba matokeo ya sasa yaliyojichomoza katika hujuma za moto sambamba na baadhi ya watu kuanza kuashiria vitisho dhidi ya wananchi wenzao walioamua kushiriki uchaguzi wa marejeo kwa kuwatilia X nyumba zao yanaonyesha safari ya hatari katika maisha miongoni mwa jamii.

0 comments:

Post a Comment