February 14, 2016

Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China inatarajiwa kuikabidhi rasmi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Hospitali ya Rufaa ya Abdulla Mzee iliyopo Wilaya ya Mkoani  Mkoa wa Kusini Pemba  mara  baada ya kukamilika ujenzi wake Mwezi Oktoba mwaka huu.
Hospitali hiyo inayojengwa  katika mfumo wa Teknolojia ya Kisasa utakaokuwa na uwezo wa kutoa huduma mbali mbali ikiwemo zile za upasuaji mkubwa, uchunguzi wa maradhi mbali mbali itaweza kukidhi mahitaji ya huduma za Kiafya kwa Wananchi walio wengi ndani ya Visiwa vya Zanzibar pamoja na  ukanda wa Mwambao wa Tanzania.
Mwakilishi wa Wahandisi wa ujenzi wa Hospitahi hiyo Bwana  Zhang Dou alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba wahandisi wa ujenzi huo kwa sasa wanaendelea kukamilisha  majengo ya huduma  tofauti, kazi itakayofuatiwa na ufungaji wa vifaa ili kukamilisha kazi hiyo kwa wakati uliopangwa.
Alisema harakati za ujenzi huo pia zinalenga kuzirekebisha Nyumba za Timu za Madaktari wa Kichina wanaopangiwa kutoa huduma mbali mbali za Afya katika Hospitali hiyo.
Bwana Zhang alisema Hospitali hiyo itakuwa na uwezo wa kulazwa wagonjwa wapatao Mia Moja na Thamanini zikiwemo huduma zote muhimu kama Vyumba Vitatu vya Upasuaji, Chumba cha wagonjwa Mahututi {ICU}pamoja na Jengo la Msikiti  litakalotumiwa naWagonjwa pamoja na familia zao kwa ajili ya Ibada.
Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alisema kwamba Jamuhuri ya Watu wa China bado inaendelea kuwa mshirika mkubwa wa Zanzibar katika kuunga mkono harakati za Maendeleo ya Wananchi wa Visiwa hivi.
Balozi Seif alisema msaada huo mkubwa wa kugharamia ujenzi wa Hospitali ya Abdulla Mzee Mkoani Kisiwani Pemba uliotolewa na rafiki wa kweli  China ni kielelezo  kinachothibitisha ushirikiano huo wa muda mrefu uliopo  kati ya China na Zanzibar.
Alisema Wananchi wa Zanzibar wanaendelea kufaidika na huduma za afya zinazotolewa na China kupitia Timu ya Madaktari wake wanaobadilishana na kutoa huduma za afya katika kipindi cha miaka miwili mfumo ambao umeanza kutekeleza kwa takriban miaka Hamsini sasa.
Ujenzi wa Hospitali ya Abdulla Mzee Mkoani  ambao ni msaada unaogharamiwa na Serikali ya Jamuhuri umekuja kufuatia ziara za mara kwa mara zinazofanywa na Viongozi wa Juu wa Zanzibar na Jamuhuri ya Watu wa China katika kuimarisha ushirikiano  wa pande hizo mbili.


Msimamizi wa ujenzi wa Hospitali ya Abdulla Mzee Mkoani 
kutoka China BwanaZhang Dou akimpatia maelezo 
Balozi Seif juu ya harakati za ujenzi
zinavyoendelea kwa ufanisi mzuri.

0 comments:

Post a Comment