January 14, 2016

Harakati za ujenzi wa  Nyumba za Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar {ZSSF} za kuwakopesha wanachama wake pamoja na kuuzwa kwa wananchi zinaendelea vizuri katika eneo la Mbweni nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar Abdulwakil Haji Hafidh amesema mradi huo ulioanza Septemba mwaka uliopita  utakaokuwa na Majumba 18 kila moja lina Ghorofa Saba lenye Fleti 252 utajengwa kwa awamu tatu tofauti  unatarajiwa kugharimu jumla ya shilingi Bilioni Arubaini na Sita { 46,000,000,000/- } hadi kukamilika kwake.
Amemueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliyefika kuangalia maendeleo ya ujenzi huo kuwa mipango  maalum imeshaandaliwa ya  jinsi nyumba hizo zitakavyotoa huduma.
Amesema baadhi zitauzwa kwa wanachama na wateja moja kwa moja, nyengine zitakodishwa kwa wateja ambao baadaye watakuwa na uwezo wa kuzinunua.
Amesema utaratibu mwengine utaandaliwa ili kuwapa fursa wanachama wa mfuko wa hifadhi ya jamii wenye kipato kidogo kukopeshwa nyumba hizo kupitia udhamini wa Benki ya Watu wa Zanzibar { PBZ } ambapo mteja anaweza kutumia kiinua mgongo chake kwa kulipia nyumba atakayoihitaji.
Naye Meneja Mipango,Uwekezaji na Utafiti wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar Khalifa Muumin Hilal  amesema majengo hayo yatajumuisha  Maduka, sehemu za burdani ya watoto pamoja na eneo maalum litakalotengwa kwa ajili ya maegesho ya vyombo vya moto sambamba  na eneo la michezo tofauti.
Kwa upande wake Msanifu Majengo anayesimamia Mradi huo Mahsen Mahd amefafanua kuwa ujenzi wa majengo hayo unazingatia taratibu zilizowekwa kwa mujibu wa sheria ikiwemo kuwashirikisha wataalamu wa Taasisi za ujenzi pamoja na watendaji wa Baraza la Manispaa sambamba na vigezo vinavyotumika katika majengo ya Kimataifa.
Akielezea matumaini ya mradi huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameushauri Uongozi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar kuhakikisha viwango vya nyumba hizo vinakuwa na fursa pana ya kuwafaidisha wanachama wa Mfuko huo wenye Vipato tofauti.
Balozi Seif alisema hatua hiyo itasaidia kuleta faraja kwa wanachama wa ngazi zote watakaokuwa na nia ya kutaka kununua, kukodi au kukopeshwa nyumba hizo kwa mujibu wa uwezo aliokuwa nao  muhusika.




0 comments:

Post a Comment