January 30, 2016

Kauli ya Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Jamal Malinzi kutoitambua kamati inayosimamia shughuli za soka visiwani Zanzibar, imewasha moto.
Itakumbukwa jana, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Malinzi alieleza msimamo wa TFF wa kuutambua uongozi wa asili wa ZFA chini ya Rais aliyemaliza muda Ravia Idarous Faina, badala ya kamati ya muda iliyoundwa kusimamia mpira wa miguu Zanzibar.
Aidha, Rais huyo alieleza kuwa TFF haiku tayari kufanya kazi na kamati hiyo na kuongeza kuwa shirikisho hilo halitahusika na lolote litakalotokea kwa ZFA chini ya kamati hiyo.
Kufuatia kauli hiyo, Makamu Rais wa ZFA aliyemaliza muda wake Haji Ameir Haji, leo Januari 29 aliitisha mkutano na waandishi wa habari katika hoteli ya Zanzibar Ocean View, na kumshutumu Malinzi, huku akimtaja kuwa sehemu ya mgogoro wa ZFA.
Ameir, al maaruf ‘Bosi Mpakia’, alisema kwa kauli yake, Malinzi ameonesha hadharani rangi zake halisi kwamba halitakii mema soka la Zanzibar na yuko tayari kushirikiana na kikundi cha watu wachache ndani ya ZFA kuhujumu soka la visiwa hivyo.
Ameir alimshangaa Malinzi kwa kuamua ‘kutia ulimi puani’, ikizingatiwa kwamba yeye ndiye aliyeitisha kikao mwishoni mwa mwaka jana kati ya uongozi wa kamati na viongozi wa juu wa ZFA jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kusafisha hali ya hewa iliyochafuka kisoka baada ya Ameir kuwashtaki mahakamani viongozi wenzake wa juu wa chama hicho.
Ameir ndiye aliyewapandisha kizimbani, Rais wa ZFA Ravia, Makamu wake anayefanyia kazi kisiwani Pemba Ali Mohammed na Katibu  Mkuu wa chama hicho Kassim Haji Salum, akiwatuhumu kwa matumizi mabaya ya fedha za chama na kuvunja katiba.
Alifahamisha kuwa,  TFF ilikutana na kamati pamoja na akina Ravia, ikiwa mpatanishi kufuatia Shirikisho la Soka Afrika kuiandikia ZFA na kuitahadharisha juu ya kesi zilizokuwa zimefunguliwa mahakamani dhidi yake kwamba zinatishia kufutiwa uanachama wake shirikisho CAF.
Alisema baada ya kikao hicho, pande zote zilikubaliana na kutoka na maazimio kadhaa, yanayozingatia ushirikiano kati yao kwa lengo la kumaliza mgogoro uliopo ambao unachangia kulipeleka kaburini soka la Zanzibar.
Aliyataja baadhi ya mambo waliyokubaliana, kuwa ni pamoja na kuiachia kamati isimamie shughuli zote za soka ikiwemo kuhakikisha ligi za madaraja yote zinachezwa, jambo ambalo tayari limefanyika.
Aidha, alisema Malinzi alipendekeza Ravia (Rais) achague watu wengine watatu kuiongezea nguvu kamati katika kazi zake za kuipitia na kuifanyia marekebisho katiba ya ZFA na hatimaye kuitisha uchaguzi mkuu.
“Kama huu si unafiki ni kitu gani. Malinzi alikuwa na maana gani kuiita kamati na ZFA Dar kama bado hana imani na upande mmoja?” alihoji.  
Ameir alisema yeye binafsi pamoja na kamati hawana tatizo na TFF kumtambua Ravia kama Rais, kwani kimsingi ZFA yenyewe sasa haipo kwani hakuna kamati tendaji ambayo kimsingi ndiyo inayoandaa mkutano mkuu na uchaguzi.
“Uongozi wa ZFA umemaliza muda tangu mwishoni mwa Disemba 2014, na hata muda walioongezewa Rais, makamu wake wawili na Katibu Mkuu nao umemalizika, lakini hakuna kamati inayoweza kuitisha mkutano mkuu, zaidi ya Mrajis wa Vyama vya Michezo kubariki kamati ya muda kusimamia soka kwa sasa,” alifafanua.
“Mimi ninajitambua kuwa si kiongozi tena wa ZFA lakini ninazungumza kama mtu mwenye kukitakia mema chama hicho tiofauti na wenzangu ambao wametegema kuchuma fedha kupitia mgongo wa mpira wa miguu,” alieleza kwa hasira.
Akizidi kuichambua kauli ya Malinzi, Ameir alisema inaonesha wazi kwamba bosi huyo wa TFF amerubuniwa na viongozi walioshtakiwa kwa lengo la kuona soka la Zanzibar linavurugika.
Ameir alikwenda mbali kwa kusema sasa anakusudia kumburuza mahakamani Rais wa TFF baada ya kutoa kauli hiyo, aliyoesema ni ya kupotosha, baada ya awali yeye binafsi kuwa msimamizi wa kikao kilichozaa muafaka ulioipa Baraka kamati, ambayo jana ameikana.   

Januari 29, 2016 

0 comments:

Post a Comment