January 15, 2016

JESHI la Polisi Mkoa wa Kusini Pemba, kwa pamoja na Chama cha Wananchi CUF, wamefikia makubaliano ya pamoja, ya kutokuwepo kwa maandamano na mkutano wa hadhara wa chama hicho, uliotarajiwa kufanyika Jumapili katika uwanja wa Tibirinzi.
Chama hicho kilitoa taarifa ya maandamano ya kuunga mkono hutuba ya Katibu mkuu wa chama chao alipozungumza na  wa waandishi wa habari pamoja na kulaani kitendo cha Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi Zanzibar, ZEC Jecha Salim Jecha kuyafuta matokeo ya uchaguzi.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana na mwandishi wa habari hizi, kikao cha kufikia mwafaka huo, kilidumu kwa saa mbili, na kujitokeza hoja nzito baina ya maofisa wa Jeshi la Polisi mkoa wa kusini Pemba na uongozi wa chama cha wananchi CUF.
Aidha taarifa hizo zinaeleza kuwa, licha ya kufikia kwa makubaliano hayo, wanachama wa chama hicho, wamepingana na uamuzi wa Jeshi la Polisi na viongozi wao, na kusema siku ikifika wataingia barabarani kwa amani kufanya maandamano.
Hata hivyo wanachama hao walisema, wanafanya hivyo, kutokana na wenzao wa chama cha Mapinduzi CCM Unguja, juzi Januari 11, waliruhusiwa kufanya maandamano ya amani, kama wanayotaka kuyafanya wao.
Katibu wa CUF wilaya ya Chakechake, Saleh Nassor Juma, alikiri kwamba baada ya kikao kizito, wamekubaliana na Jeshi la Polisi kusitisha maandamano na mkutano wa hadhara wa chama chao.
“Ni kweli tumekubaliana na Jeshi la Polisi kwamba, maandamano na mkutano yasiwepo, lakini ni kweli wanachama wetu wapinga hilo na wao wanasubiri siku ifike wafanye maandamano ya amani’’,alisema.
Katibu huyo alisema, kazi wanayoendelea kuifanya ni kuwahamasisha waatii amri ya Jeshi la Polisi, pamoja na viongozi wao wa CUF, ingawa alisema kama wakiendelea kukataa wataungana nao.
“Unajua sisi kama viongozi wa CUF, tumetii amri ya Jeshi la Polisi tusifanye maandamano na mkutano wa hadhara, na wananchama wetu tunawasisitiza sana wasishiriki, lakini kama wakiwa kicha ngumu, inabidi na sisi tuwe mbele’’,alisistiza.
Hata hivyo Katibu huyo wa CUF wilaya ya Chakechake, alisema kiliochobakia ni kuwasiliana na uongozi wa ngazi ya juu wa CUF Unguja, ili na wao watoe baraka ya kutoshiriki maandamano na mkutano huo.
Mapema Mkurugenzi mipango na uchaguzi wa chama cha CUF Omar Ali Shehe, alisema hana taarifa za kwamba Jeshi la Polisi limepiga marufuku maandamano yao ya amani, kwa vile alikuwa hajapokea taarifa hizo.
Kamanda wa Polisi mkoa wa kusini Pemba, Shehan Mohamed Shehan alisema yeye anachofahamu ni makubaliano baina yao na uongozi wa chama cha CUF ya kusitisha maandamano na mkutano huo.
Alisema, Jeshi la Polisi halina taarifa ya wanachama wa CUF kwamba wataingia barabarani kupinga amri ya viongozi wao na ya Jeshi la Polisi, na hasa baada ya kikao kizito.
“Sisi kama Jeshi la Polisi tumeshakubaliana na CUF kwamba kusiwe na maandamano wala mkutano wa hadhara wa kuunga mkono hutuba ya kiongozi wao, na tunatarajia na wanachama watii agizo hilo’’,alifafanua.

Juzi chama cha wananchi CUF kilitoa taarifa kwa waandishi wa habari kwamba, Jumapili ijayo ya Januari 17, kinatarajia kufanya maandamano ya amani yanayotarajiwa kuanzia njia ya Uwanja wa ndege na kumalizia kwa mkutano wa hadhara, viwanja vya Tibirinzi Chakechake Pemba kuunga mkono hutuba ya Katibu Mkuu wao.


: Haji Nassor, Pemba

0 comments:

Post a Comment