December 30, 2015

Watu wasiojulikana wamezichoma moto Eka Mia 150 za miwa katika Mashamba ya zao hilo ya Kiwanda cha Sukari Mahonda na kusababsisha hasara inayokadiriwa kufikia Shilingi za Kitanzania Bilioni 1.8.
Moto huo ulioshambulia  mashamba hayo jana majira ya saa sita mchana ulizimwa kwa muda wa saa tatu kwa ushirikiano kati ya wapiganaji wa Kikosi cha Zima moto na Uokozi Zanzibar, JKU, Wafanyakazi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda pamoja na Wananchi .
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amefika katika shamba hilo kuangalia hali halisi ya hasara iliyopatikana ambapo Meneja wa Mradi wa Kiwanda  hicho Tushar Mehta amesema eneo hilo la Eka hizo lilikuwa na uwezo wa kuzalisha Sukari Tani Mia 750 zenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.5.
Tushar  amesema amesikitishwa na kitendo cha watu waliofanya hujuma ya kuchoma miwa hiyo iliyokuwa ishapea licha ya Kiwanda hicho kuwekeza mradi huo wenye lengo la kuongeza mapato kwa Serikali na kuongeza fursa za ajira kwa wakaazi wa maeneo jirani yanayokizunguuka.
Kwa upande wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amesema kitendo cha kuchomwa shamba hilo la miwa Mahonda unapaswa kualaaniwa kwa vile kimeleta sura mbaya na kuisababishia ukosefu wa mapato Serikali.
Ameuomba Uongozi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda  kutovunjika moyo na kuahidi Serikali kupitia vyombo vyake vya Dola inaendelea na uchunguzi kumbaini Mtu au kikundi kilichohusika na vitendo hicho na kufikishwa kwenye vyombo vya Sheria.
Hata hivyo Balozi Seif amefahamisha kuwa Serikali itajitahidi kuendelea kuuelimisha Wananchi juu ya umuhimu wa uwekezaji vitenga uchumi nchini wenye lengo la kuimarisha ustawi wa Jamii.



0 comments:

Post a Comment