Watanzania leo wameungana pamoja kusherehekea
kilele cha maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Jamuhuri ya Tanganyika iliyojikomboa
kutoka katika Utawala wa Kingereza Tarehe 9 Disemba Mwaka 1961ambapo
imeshafikia miaka 54 sasa.
Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ambae pia ni Amiri
Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama Dr. John Pombe Joseph Magufuli
aliagiza mwaka huu Watanzania kusherehekea kwa usafi wa mazingira ili kuondoa
kabisa ugonjwa wa Kipindu Pindu.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi
aliungana na Watumishi pamoja na Wananchi wa Wilaya ya Magharibi “B” katika
usafi wa mazingira kwenye eneo la mtaro wa maji ya Mvua uliopo kwa Kira
karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Aman Karume kuelekea
Kiembe Samaki.
Sherehe za mwaka huu zimeadhimishwa kwa staili ya aina
yake kwa Watendaji na Wananchi kufanya kazi za Kujitolea katika kusafisha
mazingira kwenye maeneo na Ofisi zao kuitikia Taarifa ya Katibu Mkuu Kiongozi
wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dr. Abdulhamid Yahya Mzee ya kuwaagiza
watumishi wote wa Taasisi na Mashirika ya Umma kuripoti makazini mwao kama
kawaida.
Zoezi hilo la usafi wa mazingira lilikuwa na lengo maalum
la kuwapa fursa Wazanzibari kuungana na wenzao wa Tanzania Bara katika
maadhimisho hayo ya Uhuru wa Jamuhuri ya Tanganyika Tarehe 9 Disemba ya kila
mwaka.
Akizungumza na washiriki wa zoezi hilo la Usafi wa mazingira
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alisema umefika
wakati kwa Jamii lazima ibadilike katika kudumisha usafi wa mazingira kwa lengo
la kujiepusha na miripuko ya maradhi mbali mbali.
Balozi Seif alisema ni vyema ukaandaliwa utaratibu maalum
wa kuwapa fursa Wananchi wote kutenga siku Moja ya kila mwezi washiriki kazi za
usafi wa mazingira katika maeneo yote wanayoishi.
“ Itokee siku moja ndani ya kila mwezi kutenga muda kwa kufanya
usafi wa mazingira na hata kufunga Maduka na biashara nyengine zikasita kwa
muda ili kutoa muda japo mdogo wa kushiriki zoezi hilo muhimu “. Alisema Balozi
Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliasa kwamba tabia ya kukosa
nidhamu kwa baadhi ya watu mitaani na hata sehemu za kazi kwa kutupa taka taka
ovyo haipendezi na kwa kweli inarejesha nyuma ustawi wa Jamii.
Mapema Mkuu wa Wilaya ya Magaribi “B” Nd. Ayoub Mo’hd Mahmoud
ameupongeza Uongozi wa Mfuko wa Bara bara Zanzibar kwa jitihada zake
inazochukuwa katika kusaidia vifaa kwa ajili ya shughuli za Usafi wa
Mazingira kwenye Wilaya hiyo.
Nd. Ayoub alisema Uongozi huo wa Mfuko wa Bara bara pamoja na Watendaji
wake umekuwa ukitoa ushirikiano mkubwa kwa Ofisi yake kiasi kwamba ipo
haja kwa Taasisi nyengine kuiga mfano huo bora.
“ Tumekuwa tukishirikiana kwa karibu na Uongozi wa Mfuko wa
Bara bara katika kuimarisha usafi pamoja na utengenezaji wa Bara bara
zilizomo ndani ya Wilaya yetu “. Alisisitiza Mkuu huyo wa Wilaya ya Magharibi
“B”.
Naye kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Idara ya Utunzaji na
Utengenezaji wa Bara bara Zanzibar { UUB } Mhandisi Shomari Ali Shomari
alisema mpango maalum umeandaliwa na Idara hiyo katika kuona Bara bara itokayo
Uwanja wa Ndege hadi Mjini inakuwa katika kiwango kinachokubalika Kimataifa.
Alisema Bara bara hiyo muhimu ni kielelezo na haiba ya Mji wa
Zanzibar inayotoa sura halisi kwa wageni na watalii wanaoamua kufunga safari ya
kuitembelea Zanzibar.
Mhandisi Shomari alisema hatua hiyo imechukuliwa kwa makusudi
ili kulinda na kuhifadhi sifa halisi ya Zanzibar katika ukarimu
wake wa Kihistoria kwa wageni wanaoitembelea.
Usafi wa mazingira pia ukaonekana kushamiri ndani ya Ofisi ya
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar iliyopo Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar ambapo
watendaji wa Ofisi hiyo walijumuika pamoja katika kusafisha sehemu mbali mbali
za Jengo hilo.
Kazi hizo iliyoanza mapema asubuhi ilijumuisha watendaji wa
ngazi zote wakiongozwa na wakurungezi wa Idara zilizo chini ya Ofisi ya Makamu
wa Pili wa Rais wa Zanzibar.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa
Pili wa Rais wa Zanzibar
9/12/2015.
0 comments:
Post a Comment