December 16, 2015

Kampuni ya Uwekezaji katika Sekta ya Mafuta na Gesi kutoka Jamuhuri ya Watu wa China iko tayari kushirikiana na  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  kuendeleza miradi ya pamoja kwenye sekta hizo iwapo itapatiwa fursa katika mpango wa  uendelezaji wa miradi ya pamoja.
Mkuu wa Taaluma ya Miamba kutoka Kampuni  hiyo ya Kimataifa ya  CNOOC  Cui Hanyun akiuongoza Ujumbe wa Viongozi Watano wa Kampunin hiyo pamoja na Balozi Mdogo wa China aliyepo Zanzibar  Xie Yun Liang amesema hayo wakati wa mazungumzo yao na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Ofisini Vuga Mjini Zanzibar.
Hanyun amesema Kampuni hiyo yenye kutoa huduma katika Mataifa tofauti Ulimwenguni pia inajihusisha na uwekezaji katika Benki za Ufukweni { Off Show Banking }.
Amesema Uongozi wa Kampuni hiyo umeridhika na mazingira bora ya Visiwa vya Zanzibar na kushawishika   kutaka kuwekeza miradi yao ili kuunga mkono hatua za SMZ za kuwashawishi wawekezaji  wa ndani na nje ya Nchi kuanzisha miradi yao ya kiuchumi katika sekta tofauti Nchini.
Mtaalamu huyo wa Miamba wa CNOOC amemueleza Balozi Seif  kwamba Kampuni hiyo iko tayari kuweka nguvu zaidi katika sekta ambayo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaonyesha msisitizo kwa mujibu wa mahitaji halisi ya Taifa na Wananchi walio wengi.
Hanyun amefahamisha kwamba Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China imeshatoa baraka na kuyaruhusu Makampuni ya Nchi hiyo kuanzisha miradi ya Benki za Ufukweni kwa vile  tayari imeshakuwa na wataalamu na uzoefu wa kutosha wa miaka mingi kwenye sekta hizo.
Naye Meneja wa Biashara wa Kampuni hiyo Ukanda wa Bara la Amerika Hu Gencheng alieleza kwamba Kampuni hiyo mbali ya uzalishaji pia imekuwa ikipokea Gesi  kutoka Mataifa ya Indonesia, Qatar, na Autralia.  
Kwa upande wa Bara la Afrika Gencheng  alisema CNOOC iko katika uendelezaji wa miradi ya Benki za Ufukweni  katika  Mataifa ya Nigeria, Equitorial Guinea, Congo Brazaville, Kenya na Uganda.
Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameueleza ujumbe huo wa Kampuni ya Kimataifa ya uwekezaji wa Mafuta na Gesi ya China kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  imeshajidhatiti katika kutoa ushirikiano wa kina kwa Taasisi au Kampuni ye yote iliyoonyesha nia ya kutaka kuwekeza miradi yao ya Kiuchumi Zanzibar.
 “ Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kutoa ushirikiano wa Karibu katika kuona malengo ya Kampuni ya CNOOC yanafanikiwa vyema “. Alisema Balozi Seif.
Amesema Suala la Mafuta na Gesi kwa  sasa tayari limeshapatiwa maamuzi na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutolewa ndani ya Mambo ya Muungano ili kuipa fursa pana Zanzibar kushughulikia yenyewe katika dhana nzima ya kujiimarisha Kiuchumi.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  amesema Zanzibar itaanza matayarisho kamili ya umiliki wa Sekta hiyo pamoja na Kuunda Shirika litakaloshughulikia Sekta ya Mafuta na Gesi mara baada ya kukamilika rasmi kipindi cha mpito cha uchaguzi Mkuu wa Zanzibar.






Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
16/12/2015.


0 comments:

Post a Comment