February 07, 2016

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ametoa wito kwa Majaji na Mahakimu Nchini kuacha kugugumizi katika utoaji wa haki ili kuondoa au kupunguza zaidi muda mrefu  unaochukuliwa katika kutoa hukumu kwa kesi zinazopelekwa Mahakamani.
Amesema kigugumizi hicho mbali ya kulalamikiwa kwa kipindi kirefu na Wananchi   walio wengi lakini pia kinachangia sana kuuondolea  heshima yake Muhimili huo ukiwa miongoni mwa  Mihimili Mitatu ya Dola.
Balozi Seif Ali Iddi ametoa wito huo wakati akizungumza na Majaji, Wanasheria na Mahakimu ndani ya Jumla la Sheria Zanzibar baada ya kuyaongoza Matembezi ya maadhimisho ya Siku ya sheria yaliyoanzia Mahakama Kuu Vuga kupitia Benbella, Michenzani, Kituo cha Polisi madema na kumalizikia katika Viwanja vya Michezo vya Maisara Mjini Zanzibar.
Amesema zipo kesi zinazolalamikiwa na Wananchi walio wengi kama Dawa za kulevya na udhalilishaji wa Kijinsia unaowakumba zaidi watoto wadogo na wanawake zinazopelekwa Mahakamani lakini hatma yake inaishia hewani na wahusika kuwaona wakiendelea kutanua mitaani.
Balozi Seif ameeleza kwamba ushahidi wa wazi katika baadhi ya kesi zinazopelekwa kwa Mahakimu hutolewa na wahusika lakini kinachojitokeza kwa baadhi ya Majaji na Mahakimu kueleza kuwa ushahidi bado haujakamilika.
Katika kukabiliana na vitendo hivyo Balozi Seif amewakumbusha watendaji wa Mahakama kubeba jukumu lao kwa kuchukuwa hatua za haraka za kutoa maamuzi ili kupunguza mrundikano wa majalada ya kesi yaliyopo mezani kwao.
“ Majaji na Mahakimu wanapaswa kujiepusha na malalamiko ya mrundikano wa mashauri yanayowahusu ambayo yamekuwa yakilalamikiwa sana na Wananchi ”. Amesema Balozi Seif.
Akizungumzia suala la mazoezi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alitahadharisha kwamba kitendo cha watumishi wa Sheria kukaa maofisini kwa muda mrefu na baadae kuishia nyumbani bila ya kufanya mazoezi ni hatari kwa afya zao.
Amesema ni vyema kwa watumishi hao kujipangia utaratibu muwafaka wa kufanya mazoezi ya viungo hata kwa siku moja ndani ya wiki ikiwezekana sio mbaya kuyafanyia nyumbani iwapo muda wa kufanya hivyo umekuwa finyu.
Balozi Seif alieleza kwamba mazoezi ni afya kubwa inayomsaidia Jaji, Mwanasheria na Hakimu kufikiri  vyema katika utekelezaji wa jukumu lake zito kwa Umma.
Mapema akimkaribisha mgeni rasmi katika falya hiyo Jaji Mkuu wa Zanzibar Mh. Omar Othman Makungu maadhimisho ya Wiki ya Sheria Zanzibar yameamua kuingiza matembezi  kwa mara ya kwanza katika ratiba yake ili kutoa fursa kwa watendaji wa taasisi hiyo.
Jaji Mkuu Makungu alisema miili inahitaji mazoezi na hata matembezi na ilionekana na Uongozi wa Mahakama Kuu kutokana na watendaji waliowengi wanakaa muda mrefu maofisini jambo ambalo ni hatari kwa afya zao.

Alisema changamoto hii ya ukosefu wa kufanya mazoezi kwa baadhi ya watendaji wa Sekta ya Sheria itatoa ushawishi kwao kuanza ukurasa mpya wa kuamua kujiingiza kwenye eneo hilo muhimu.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi
kati kati akiongoza matembezi ya kuadhimisha siku ya Sheria
Zanzibar yalioanzia Mahakama Kuu Vuga Mjini Zanzibar
na kuishia Viwanja vya Maisara.
 

Baadhi ya Vikundi vya mazoezi vikipasha mwili katika 
Viwanja vya Maisara Suleiman baada ya kukamilisha 
matembezi ya siku ya Sheria Zanzibar.

0 comments:

Post a Comment