December 05, 2015


Wahitimu wa Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar wamehimizwa kuwa tayari kufanya kazi popote  watakapopangiwa kwani wanawajibu wa kuchangia jitihada Serikali katika kupambana na maradhi mbali mbali yanayoisumbua jamii.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohammed Shein ametoa rai hiyo katika Mahafali ya 22 ya Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar huko Mbweni nje kidogo ya Mji wa Zanzibar katika hotuba yake ilisomwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idi.
Amesema kuna baadhi ya baadhi ya wahitimu wanaoajiriwa na Wizara ya Afya wanapiga chenga kufanya kazi Kisiwani Pemba wakisahau kwamba Wananchi wa kisiwa hicho pia wanahitaji kupata huduma zao.
Amesema watumishi wa Umma wakiwemo wa sekta ya afya wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria na taratibu za kazi na miongozo ya sehemu wanazoajiriwa na ni vizuri wawe mfano wa tabia njema kwa kushikamana katika kutekeleza maadili ya kazi zao.
“ Nimefurahi kusikia kuwa katika orodha ya wahitimu wetu wa fani za afya chuoni hapa wapo waliotoka Tumbatu, Kojani, Fundo, Mtende, na Maeneo mengine ambayo watu wengi huwa wanaona tabu kwenda kufanya kazi kutokana na mazingira ya Kijiografia yaliyopo “. Amesema Dr. Shein.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pia aliiagiza Wizara ya Afya kufanya tathmini ya mahitaji ya wataalamu wa afya katika maeneo hayo ili kujua changamoto zilizopo na kuchukuwa hatua za haraka  zitakazowezesha vijana kutoka maeneo hayo kuajiriwa.
Akizungumzia suala la uwekezaji katika sekta ya Afya Zanzibar Rais Shein amesema Serikali imekuwa ikishajiisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuja kuwekeza katika sekta hiyo muhimu ili kusaidia katika kuimarisha huduma za afya Nchini.
Rais wa Zanzibar amewasisitiza wahitimu wa Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar kuchangamkia ajira zinazotolewa na Serikali na Sekta Binafsi wakitambua kwamba Hospitali zote zina lengo la kuimarisha huduma za afya kwa faida ya Wananchi.
Mapema Mkuu wa Chuo cha Taalum za Sayansi za Afya Zanzibar Dr. Haji Mwita Haji amesema Uongozi wa Chuo hicho kupitia Baraza lake umeamua kuongeza majengo zaidi ili kuwahudumia vyema wanafunzi wanaoamua kujiunga na chuo hicho sambamba na mahitaji ya ongezeko la Hospitali na vituo vya Afya Nchini.
Akimkaribisha Mgeni rasmi katika ufungaji wa Mahafali hayo ya 22 ya Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar, Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Mh. Mahmoud Thabit Kombo  amewaomba wauguzi kufuata maadili  ya kazi zao ili kuondosha malalamiko yanayotolewa na wananchi juu ya lugha zao kwa wagonjwa .
Jumla ya wahitimu 440 wamefanikiwa kupata stashahada katika fani saba za sekta ya afya ikiwemo Afisa Tabibu wa Afya ya Kinywa na Meno, Afisa Tabibu, Afya ya Mazingira, Uuguzi na Ukunga, Utabibu wa Maabara,Madawa pamoja na  Ufundi Sanifu wa Vifaa vya Hospitali.

0 comments:

Post a Comment