November 19, 2015


Wagombea wa urais Zanzibar wametakiwa kuwa na moyo wa subira na kutoa nafasi kwa mazungumzo yanayoendelea ya kusaka muafaka wa mgogoro wa uchaguzi wa Zanzibar baada ya matokeo kufutwa Oktoba 28, mwaka huu. 
Wito huo ulitolewa na mgombea wa urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Tadea, Juma Ali Khatib, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na mazungumzo ya kusaka muafaka yanayofanywa na viongozi wa kitaifa wakiwamo marais wastaafu visiwani humo.
Khatibu alisema mazungumzo yanayofanyika yana umuhimu mkubwa katika kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa uchaguzi kwa manufaa ya Zanzibar na wananchi wake.
 “Zanzibar inapita katika wakati mgumu wa kisiasa na kiuchumi kutokana na hali ya maisha ya wananchi kubadilika tangu kuibuka kwa mgogoro wa uchaguzi Oktoba 28 mwaka huu.”
Alisema hali ya biashara Zanzibar imetetereka na kusababisha mfumuko mkubwa wa bei za bidhaa na kuwataka wananchi pamoja na kuwapo hali hiyo kuendeleza kudumisha amani na umoja wa kitaifa wakati viongozi wa kitaifa wakitafuta muafaka wa mgogoro huo. 
“Sie kama wagombea ni muhimu tuwe na moyo wa subira, tuyape nafasi mazungumzo ya kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa Zanzibar,” alisema Khatibu ambaye alikuwa akiwania urais wa Zanzibar kwa mara ya tatu. 
Hata hivyo, alikosoa akisema  haikuwa sahihi mazungumzo ya kusaka muafaka wa uchaguzi wa Zanzibar kushirikisha wagombea wawili, Dk. Ali Mohamed Shein wa CCM na Maalim Seif Sharif Hamad wa Cuf kati ya 14 waliopitishwa na Zec kuwania wadhifa huo.
Alisema wagombea wote walikuwa na sifa na haki sawa, hivyo haikuwa sahihi kutengwa katika meza ya mazungumzo baada ya Mwenyekiti wa Zec, Jecha Salim Jecha,  kufuta matokeo ya uchaguzi.
:Nipashe

0 comments:

Post a Comment