November 19, 2015


Serikali imepiga marufuku uuzaji na ununuzi wa karafuu usio rasmi (vikombe) kuepusha wizi wa zao hilo mashambani na ukataji wa mikarafuu unaofanywa na baadhi ya watu kutokana na kuzoeleka kwa biashara hiyo.
Wakizungumza katika nyakati tofauti Wakuu wa Wilaya za Unguja na Pemba wamesema hakuna ruhusa kwa mtu yoyote kuuza au kununua karafuu mbichi au kavu na atakaebainika kujihusisha na biashara hiyo atashughulikiwa ipasavyo.
Wamebainisha kuwa Serikali haiwezi kuvumilia makosa hayo kwa sababu wanaofanya uhalifu huo hawana imani na Serikali haina imani nao hivyo kwa watakaokamatwa watachukuliwa hatua kwa misingi ya kisheria.
Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini ‘B’ Haji Makungu Mgongo amesema  
karafuu ni zao la uchumi wa Taifa hivyo Wilaya hiyo  haitokuwa tayari kuona baadhi ya watu wakihujumu kwa wizi hasa kukata mkarafuu kwa tamaa ya kupata maslahi ya muda mfupi.
 Nae Mkuu wa wilaya ya Wete Hassan Khatib Hassan ameshauri kurejeshwa kwa utamaduni wa uchumaji karafuu kwa kambi kwani kufanya hivyo kutapunguza uhalifu unatokea katika mashamba yao.
Mwanasheria wa Shirika la ZSTC Ali Hilal Vuai amesema kuiba karafuu ama kukata mikarafuu  kwa matumizi mengine  yoyote ni makosa kwa mujibu wa sheria namba 2 ya Maendeleo ya Karafuu ya mwaka 2014.
Amesema  sheria hiyo inakataza  kuihujumu mikarafuu kwa aina yoyote ile na atakaebainika kufanya vitendo hivyo anapaswa kupelekwa katika vyombo vya sheria.

0 comments:

Post a Comment