November 21, 2015

Mkuu wa Chuo cha Habari Zanzibar Dkt. Aboubakar Rajab
akitoa hutuba ya ufunguzi katika Mkutano Mkuu wa Wadau wa 
Jumuiya ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC) mjini Zanzibar, 
Kulia ni Katibu wa Tume ya Utangazaji Zanzibar Chande Omar 
na kushoto ni Mwenyekiti wa ZPC Abdallah Mfaume.
Waandishi wa habari Zanzibar wametakiwa kufuata maadili na miongozo ya taaluma zao bila ya kujali vikwazo na changamoto zinazowakabili katika utendaji wa majukumu yao.
Hiyo ni hatua ya kuifanya jamii iendelee kuunga mkono juhudi zinazofanywa na waandishi hao katika nyanja mbali mbali za kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Mkuu wa Chuo cha Uandishi wa Habari Zanzibar, Dkt. Aboubakar Sheikh Rajab amesema kuwa endapo waandishi wa habari watashindwa kuzingatia maadili yao kutokana na changamoto za kiutendaji fani hiyo itapoteza thamani na heshima yake ya kujenga jamii na maendeleo ya nchi.
Akizungumza katika mkutano wa wadau wa Klabu ya waandishi wa habari Zanzibar ZPC ameeleza kuwa kuna baadhi ya waandishi wa habari wanatumiwa vibaya na baadhi ya vyama vya kisiasa katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu jambo ambalo ni kinyume na misingi ya maadili yao.
 " Waandishi lazima kwanza tufikie wakati tutambue kuwa asili ya kazi yetu ni kujitolea kwa jamii licha ya kuwa hali zetu za kipato ni ndogo lakini tusikubali wanasiasa na watu wenye uwezo kutumia udhaifu huo kutusababisha tuvunje maadili yetu.
Akitoa mada ya umuhimu wa waandishi wa habari kuzingatia maadili ya uandishi wa habari na utangazaji, Katibu Mkuu wa Tume ya Utangazaji Zanzibar Chande Omar Omar amesema waandishi wa habari wanaofuata maadili wanakuwa na fursa pana ya kuepuka vikwazo na lawama kutoka kwa jamii.
" Mnatakiwa kujua kuwa hamfanyi kazi kwa ajili yenu bali mnafanya kazi kwa ajili ya jamii nzima hivyo ujumbe mnaotoa kupitia vyombo nyenu kwanza mkae na kuupitisha katika tanuru la kitaaluma na maadili badae ndiyo mpate kuutuma kwa jamii.
“Mnatakiwa kuepuka masuala ya udini,ukabila,utaifa,rangi ya mtu jinsia na hali ya kiuchumi na kijinsia bali kila kundi mlipe haki yake kwa lengo la kuhakikisha Zanzibar inaendelea kuwa nchi yenye amani na utulivu wa kupigiwa mfano.",alisema Omar.
Kwa upande wake mshiriki wa mkutano huo, mwakilishi kutoka Chama cha TADEA Zanzibar, Juma Ali Khatib amewataka waandishi wa habari kutumia kalamu zao kufafanua kwa kina upotoshwaji wa sheria unaofanyika Zanzibar kwa sasa tangu Tume ya uchaguzi nchini ilipofuta matokeo ya uchaguzi mkuu.
Mkutano huo umefikia maazimio ni pamoja na waandishi wa habari Zanzibar kuendelea kufuata maadili ya fani hiyo kwa wakati wote na kuhamasishana kusoma Katiba za nchi pamoja na sheria mbali mbali ili waweze kuwa na uelewa mpana wa masuala ya kisheria wanapotoa taarifa zao.

Is-haka Omar, Zanzibar.

0 comments:

Post a Comment