November 22, 2015


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

Zanzibar                                                                                                                                                 22 Novemba, 2015 
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein jana alikagua shughuli mbalimbali za miradi ya uwekezaji katika maeneo huru ya Fumba nje kidogo ya mji wa Zanzibar na kueleza kuridhishwa  kwake na kasi ya uendelezaji wa miradi aliyoitembelea.
“haya ndio maendeleo tunayoyataka na hatuna budi kuyatangaza ili watu walijue eneo hili la Fumba lenye mwelekeo mpya kabisa wa maendeleo ya kisasa” alisema Dk. Shein.
Katika ziara hiyo alitembelea Mradi wa Maendeleo ya Mji wa Fumba (Fumba Uptown Living Project) unaojumuisha ujenzi wa nyumba 500 za aina na ukubwa tofauti pamoja na huduma nyingine za kijamii,ujenzi wa gati ndogo na mitambo ya ujenzi wa barabara.
Mradi huo unajengwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na Makampuni ya Bakhresa (Said Salum Bakhresa Group of Companies). 
Dk. Shein aliupongeza uongozi wa Makampuni ya Bakhresa chini ya kiongozi wake Sheikh Said Bakhresa kwa kuonesha mfano katika uwekezaji katika mradi huo mkubwa ambao sio tu utaibadilisha kabisa haiba ya mji wa Fumba lakini kuipatia sifa zaidi Zanzibar.
Akitoa maelezo kwa Mheshimiwa Rais, Mwenyekiti wa Makampuni ya Bakhresa Sheikh Said Salum Bakhresa alieleza kuwa awamu ya kwanza ya mradi huo utakaogharimu zaidi dola za kimarekani milioni100, utahusisha ujenzi wa nyumba 100 utakaoanza mwezi ujao.
Alifafanua kuwa katika kurahisisha usafirishaji wa vifaa vya mradi huo, kampuni yake itajenga gati ndogo ambayo itawezesha vifaa na mahitaji mengine ya mradi kwenda moja kwa moja Fumba.
Hata hivyo aliongeza kuwa baada ya mradi kukamilika bandari hiyo itaimarishwa ili itumike kwa shughuli za kusafirishia abiria na mizigo kwa boti za kampuni yake na nyingine kati bandari za Zanzibar na maeneo mengine ya Pwani ya Afrika Mashariki.
Mbali na nyumba sehemu ya mji huo hasa sehemu ya kilomita 2 inayotazamana na bahari itajengwa sehemu za kupumzikia wakaazi na wageni watakaotembelea eneo hilo, sehemu za burudani, michezo ya watoto, mikahawa, maduka na michezo ya maji (water park).
Sheikh Said Bakhresa alisema anaamini kuwa kuanza kwa ujenzi huo kutavutia wawekezaji wengi zaidi kuja katika eneo hilo na kwamba hana shaka yeyote baada ya miaka michache ijayo sehemu hiyo itakuwa mashuhuri kama sehemu nyingine maarufu duniani.
Katika maelezo yake hayo, aliipongeza na kuishukuru Mamlaka ya Kuendeleza Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) kwa ushirikiano wao wa karibu na kuongea kuwa hivi sasa mamlaka hiyo imepunguza urasimu na kuongeza ufanisi. Alizishukuru pia mamlaka nyingine kwa ushirikiano wao ambao umewezesha mradi huo kuanza utekelezaji wake.
Awali akitoa maelezo kwa Mkurugenzi Mkuu wa ZIPA Ngd.  Salum Khamis Nassor alisema utaratibu wa sasa maombi ya mradi yanapaswa kujibiwa ndani wiki mbili na ofisi yake imekuwa ikiutekeleza utaratibu huo ipasavyo.
Kuhusu ujenzi wa miundombinu ya barabara katika eneo hilo la uwekezaji la Fumba, Mkurugnezi Mkuu huyo alibainisha kuwa barabara zenye urefu wa kilomita 12 zimo mbioni kujengwa kuzunguka mradi huo hivyo kujenga mazingira mazuri ya uwekezaji.   
Alibaisha pia kuwa Taasisi yake kwa kushirikiana na Kampuni ya Bakhresa inajenga kituo cha habari katika mlango wa kuingilia eneo hilo ili kutoa taarifa na kuelimisha wananchi kuhusu shughuli zinazofanyika katika eneo hilo ikiwa na pamoja na fursa zilizomo ambazo wanaweza kufaidika nazo.
Hatua hiyo alisema ni sehemu ya jitihada za kujenga maelewano mazuri na jamii ili kupunguza misuguano kati ya wawekezaji na jamii.
Katika ziara hiyo Dk. Shein alikagua ujenzi wa barabara kutoka Skuli ya Bwefum hadi Kiwanda cha Maziwa cha Bakhresa yenye urefu wa kilomita 2.7 na upana wa mita 50 pamoja na mtambo wa kupikia lami na mashine ya kusaga kokoto.
Barabara hiyo inajengwa na Kampuni ya Ujenzi ya Coastal Dredging Company Tz Ltd ambayo ni kampuni tanzu ya makampuni ya Bakhresa ambayo inajenga miundombinu katika mradi huo.
Kwa mujibu wa Mkurungezi Mkuu wa Kampuni hiyo Ali Haroun Suleiman mtambo wa kupika lami una uwezo wa kupika kati ya tani 100 hadi 110 za lami kwa saa wakati mashine ya kusaga kokoto (crusher) ina uwezo wa kusaga kokoto tani 120 kwa saa.
Kampuni ya Bakheresa tayari imejenga kiwanda kikubwa cha maziwa katika eneo hilo ambacho kinasemekana ndio kiwanda kikubwa kabisa cha aina hiyo Afrika Mashariki.
Katika ziara hiyo Dk. Shein alifuatana na viongozi mbali mbali wa serikali akiwem Waziri wa Ardhi, Makazi, Maji na Nishati Mheshimiwa Ramadhani Abdalla Shaaban na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ Mheshimiwa Haji Omar Heri.
  
Postal Address: 2422 Tel.+255 776 613 015, Fax: 024 2231822 

0 comments:

Post a Comment