May 15, 2014


STATE HOUSE ZANZIBAR

OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

    Zanzibar                                                                                                         15 Mei, 2014

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza dhamira ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuendeleza na kuimarisha ushirikiano na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo(IFAD).

 Dhamira hiyo amesema inatokana na ukweli kuwa miradi inatekelezwa kwa ushirikiano na mfuko huo humu nchini inakwenda sambasamba na utekelezaji wa Dira Zanzibar ya 2020 na Mpangomkakati wa Serikali wa kuimarisha kilimo nchini.
Akizungumza na ujumbe wa Bodi ya Utendaji ya Mfuko huo ulioongozwa na Dk. Yaya Olaniran Ikulu leo, Dk. Shein amesema kwamba Serikali na wananchi wa Zanzibar wana matumaini makubwa na ushirikiano na Mfuko huo kwa kuwa ushirikiano huo umekuwa wa manufaa makubwa kwa wakulima wa Zanzibar.
 
“Azma yetu ni kuendelea kufanyakazi na IFAD kwa kuwa malengo ya msaada wenu yanasadifiana na malengo yetu ya mipango yetu mikuu kama vile Dira ya Maendeleo na Mpangomkakati wetu wa kuimairsha kilimo ambayo yamelenga katika kujihakikishia usalama wa chakula na kuondoa umasikini” alieleza Dk. Shein.

Katika mazungumzo hayo Mhe Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliueleza ujumbe huo kuwa Serikali katika kuhakikisha wakulima wanapata huduma nzuri za kitaalamu imeamua kuimarisha taasisi ya Utafiti ya Kizimbani hivyo ingependa kuona taasisi hiyo inafaidika pia na misaada kutoka mfuko huo.

 “Tumeamua kukipandisha hadhi kituo chetu cha utafiti kuwa taasisi ili kutoa huduma bora zaidi kwa wakulima wetu na katika eneo hili la utafiti tungependa kushirikiana zaidi na IFAD kukiwezesha kituo kujenga uwezo kwa kukipatia mindombinu ya utafiti pamoja na taaluma”alisema Dk. Shein na kuongeza kuwa kwa kufanya hivyo itakuwa msaada mkubwa kwa wakulima.

 Aliueleza ujumbe huo kuwa binafsi anaamini kama inavyoamini Bodi ya Mfuko huo kuwa ushirikiano huo una fursa ya kuleta mabadiliko makubwa sio tu kwa wakulima bali kwa ustawi wa wananchi wote wa Zanzibar.

“Nimefurahi kuwa ziara hii itawakutanisha na wakulima wetu na kujiona wenyewe jinsi wanavyofanyakazi na kunufaika na misaada ya IFAD na kwa hakika ni fursa pekee ya kuona namna Mfuko unavyoleta mabadiliko kwa wakulima wetu”Dk. Shein alisema.

Alitumia fursa hiyo kuishukuru Bodi ya Mfuko huo na uongozi wa IFAD kwa kufanyakazi kwa karibu na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kubainisha kuwa uhusiano huo umekuwa wa manufaa kwa wakulima na jamii ya watanzania kwa ujumla.

Akitoa maelezo kuhusu ziara yao hiyo Kiongozi wa Ujumbe huo Dk. Yaya Olaniran alisema kuwa ujumbe huo upo nchini kutembelea miradi mbalimbali inayofadhiliwa na Mfuko ambapo tayari wameshatembelea miradi iliyo Tanzania Bara.
Alibainisha kuwa lengo la ziara hiyo ni kuuwezesha Mfuko huo kujionea hali halisi ya miradi hiyo na kukutana wahusika mbalimbali wakiwemo wakulima ambao ni walengwa wakubwa wa miradi hiyo.

“Kwa kutembelea miradi hii na kuona hali halisi pamoja na kuzungumza na wakulima wadogo wadogo kujua ufanisi na changamoto zake kutaisaidia mijadala katika Bodi na kufanya maamuzi yanayoendana na uhalisia wa maendeleo ya miradi tunayoifadhili” alisema Dk. Yaya.
Alieleza kuwa ushirikiano kati ya IFAD Serikali zote mbili umekuwa mzuri na kwamba hadi sasa Mfuko huo umetumia dola milioni 360 kusaidia wakulima katika miradi mbalimbali ya kilimo nchini Tanzania.  
“Miradi yetu imelekezwa katika sekta hii ya kilimo ambayo inategemewa na wananchi wengi katika nchi zetu lengo ni kuinua uchumi na kupunguza umasikini” alieleza na kufafanua kuwa IFAD inaamini kuwa kufanya hivyo kutasadia pia kupunguza tatizo la ajira kwa vijana.
Miongoni mwa waliofuatana na Dk. Yaya ni Katibu wa Mfuko huo Bwana Rasit Pertev, Mkurugenzi wa Mfuko huo Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika Bwana Perin Sante Ange, Mwakilishi wa Mfuko huo Tanzania bwana Francisco Pichon, Mkuu wa Programu kwa Tanzania Dk. Mwatima   Abdalla Juma  pamoja na wajumbe wawili wa Ofisi ya Tathmini ya IFAD.   

 

0 comments:

Post a Comment