May 24, 2014


SERIKALI ya Zanzibar imetiliana saini na kampuni ya ‘JiangSu Provincial Construction Group Co. Ltd’ ya kutoka Jamhuri ya Watu wa China, makubaliano ya ujenzi na utanuzi wa hospitali ya Abdalla Mzee iliyoko Mkoani Pemba.
Hafla ya utiaji saini huo ilifanyika katika Wizara ya Afya, ambapo Zanzibar iliwakilishwa na Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dk. Mohammed Saleh Jidawi, wakati Naibu Meneja wa kampuni hiyo Dai Houxing alisaini kwa niaba ya kampuni  yake.
Akitoa shukurani kwa Serikali ya China, Dk. Jidawi alisema hatua hiyo inadhihirisha kuimarika kwa uhusiano na udugu wa miaka mingi kati ya China na Zanzibar, ambao umesaidia sana maendeleo ya visiwa vya Unguja na Pemba.
Dk. Jidawi alisema ujenzi huo utaibadilisha kabisa hospitali hiyo na kuwa ya kisasa zaidi ikiwa na huduma zote muhimu ikiwemo CT Scan, chumba cha kuhifadhia maiti, jiko la kuchomea taka, idara ya maradhi ya dharura, kitengo cha uangalizi maalumu (ICU), maabara na nyenginezo.
Aidha alisema, hatua hiyo itawezesha kuipandisha daraja na kuwa hospitali ya rufaa kwa upande wa Pemba.
Alifahamisha kuwa kazi za ujenzi wa hospitali hiyo zinatarajiwa kuanza mwezi moja tangu siku ya utiaji saini makubaliano hayo, na umekisiwa kukamilika baada ya miezi 25.        
Katibu Mkuu huyo alisema matengenezo hayo makubwa yatagharimu dola za Kimarekani milioni 13, ambazo zote zitatolewa na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China.
“Ni wazi kwamba hospitali ya Abdalla Mzee sasa imekuwa ndogo kutokana na ongezeko kubwa la watu kulinganisha na wakati ilipojengwa zaidi ya miaka 40 iliyopita,” alisema Dk. Jidawi.
Alisema makuabaliano ya kuifanyia matengenezo hospitali hiyo yalitokana na ziara ya Rais wa China Mhe. Xi Jinping hapa Tanzania mwezi Machi mwaka huu, ambapo alipata fursa ya kuzungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.
Halikadhalika alisema ziara ya Dk. Shein aliyoifanya mwezi Mei 2013 nchini China, nayo imechangia pakubwa kwa nchi hizo kukubaliana kufanyika kwa ujenzi huo.
Alizishukuru serikali zote mbili, pamoja na zile za Mkoa na Wilaya ya Kusini Pemba, na watendaji wote wa wizara yake kwa kufanikisha kufikiwa kwa hatua hiyo.
Kwa upande wake, Balozi Yunliang ambaye alishuhudia utiaji saini huo, alieleza matumaini yake kuwa kazi hiyo itafanyika kwa kiwango bora kutokana na uzoefu mkubwa na wa miaka mingi ilionao kampuni ya JiangSu Provincial Construction Group Co. Ltd ya China.
Alisema nchi yake inaona fahari kuendelea kuisaidia Zanzibar ambayo imejenga nayo urafiki mkubwa tangu ilipojikomboa kwa Mapinduzi ya mwaka 1964.  
Naye Naibu Meneja wa kampuni ya JiangSu anayeshughulikia miradi ya nje Dai Houxiang, aliahidi kuwa kazi hiyo itamalizika kwa wakati, huku akiomba wananchi wa Pemba waipe ushirikiano kampuni yake wakati wote wa ujenzi huo.  
Alisema kampuni yake ina uzoefu wa takriban miaka 60 ikiwa imefanya kazi katika nchi mbalimbali za Afrika na kujipatia umashuhuri mkubwa.
Hatua hiyo imekuja siku mbili tu baada ya China na Zanzibar kusaini ujenzi wa kitengo cha uangalizi maalumu (ICU) katika hospitali kuu ya Mnazimmoja.
 
Balozi Mdogo wa China Zanzibar Xie Yunliang (wa pili kushoto), akitoa maelezo kwa baadhi ya viongozi wa Wizara ya Afya waliongozwa  na Katibu Mkuu Wizara ya Afya mara baada ya utiaji saini makubaliano ya ujenzi wa  Hospitali ya Abdulla Mzee Pemba utakaoanza mwezi ujao. (Picha na Makame Mshenga wa Maelezo Zanzibar).
Naibu Meneja wa kampuni ya JiangSu Provincial Construction Group Co. Ltd Dai Houxiang akielezea mikakati ya ujenzi huo utakaoanza mwishoni mwa mwezi ujao ambao unatarajiwa kukamilika baada ya miezi 25. Kulia ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dk. Mohammed Jidawi. Ujenzi huo utagharimu Dola za Kimarekani milioni 13.
 

0 comments:

Post a Comment