March 08, 2016

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba Mhe: Mwanajuma Majid Abdallah, amewataka wananchi Kisiwani Pemba, kushirikiana kikamilifu katika kutokomeza vitendo vya udhalilishaji, wanavyofanyiwa wanawake na watoto katika jamii.
Alisema kuwa, katika kulitokomeza hilo ni lazima jamii iondoe woga na kuona haya, pia kuepusha rushwa na vishawishi vyate ambavyo hukiuka haki na misingi ya kibinaadamu.
Mkuu huyo wa Mkoa aliyaeleza hayo, wakati akizungumza na wananchi wa mikoa miwili ya Pemba, katika maadhimisho ya siku ya wanawake duniani, aliyofanyika katika uwanja wa Gombani Wilaya ya Chake Chake Pemba.
Aidha alisema hali ya wanawake kwa sasa imejaa matatizo mengi ya aina mbali mbali ikiwa ni pamoja na umasikini uliokithiri na uvunjaji wa Sheria zinazowahusu.
"Siku hii wanawake hupata fursa ya kuangalia mafanikio na matatizo changamoto, Sote kwa pamoja tunatakiwa kuwa makini na kusimamia kuondoa vitendo hivyo vionevu na unyanyasaji wa mwanamke" alisema.
Alisema suala la ukatili kwa wanawake hujumuisha mambo ya kupigwa, kufungwa, kubakwa, kukatwa sehemu za mwili, kukatishwa masomo, kuozeshwa waume katika umri mdogo kutumikishwa kusikokuwa na mipaka na kutojali utu.
Hata hivyo alisema ni vyema kukumbusha vyombo vyote vinavyosimamia ustawi na haki za mwanamke na watoto, hasa vyombo vya Sheria kusimamia na kuhakikisha vitendo vya ushalilishaji vimepotea katika jamii.
Aidha alivitaka vyombo vya sheria kusimamia vyema haki za wanawake na kuhakikisha wanastahili kupewa haki zao wanapewa bila ya hofu yoyote.
Aliwataka wanawake wenzake kuacha tabia ya kujidhalilisha wenyewe, wakati wanapofuata haki zao wanapaswa kufuata taratibu, mila na desturi  na silka za mzanzibari.
Hata hivyo aliwataka wananchi, vyombo vya dola kushirikiana na kushikamana katika kuhakikisha vitendo vyote vya udhalilishaji vinatokomezwa.
Naye mkuu wa Wilaya ya Chake Chake Pemba, Mhe:Hanuna Ibrahim Masoud, aliwataka wanawake kujitokeza kupinga vitendo vya udhalilishaji wanaovyofanyia majumbani na mitaani, ili kuhakikisha wanaofanya vitendo hivyo wanatiwa hatiani.
Alisema tayari kuna baadhi ya vijiji vimekuwa vikiwakandamiza wanawake, katika kupata haki zao ikiwemo wanaume wanaokwenda agoni kukataa kupima afya zao wanaporudi majumbani mwao.
“Mwanamme anakaa miezi miwili au mitatu halafu akirudi akiambiwa kupima hataki, huu pia ni udhalilishaji kwani hujuwi nini huko anachikifanya”alisema.
Kwa upande wake Afisa Mdhamini wa Uwezeshaji Ustawi wa Jamii Vijana Wanawake na Watoto Mauwa Makame Rajab, alisema wanawake ndio washiriki wakuu katika kuinua nchi yao kiuchumi pia ndio walezi wa familia.
Alisema Serikali imechukua juhudi kubwa ya kijenga Wizara, kuifanyia marekebisho Sera ya mwaka 2011 na kutaarisha vipindi mbali mbali ambavyo vinashajihisha kuleta maendeleo.
Alisema bado wanawake wamekuwa wakikumbana na changamoto mbali mbali, ikiwemo Uwelewa mdogo  katika jamii, ikiwemo mambo ya sheria, urasimu katika majumbani, vyombo vya sheria pamoja na baadhi ya sheria kuwa kandamizi ikiwemo sheria ya Ndoa ya mwaka 1971.
Nae Ashloo Massoud wakati alipokuwa akisoma Risala katika maadhimisho hayo alisema, wanawake bado wanakabiliwa changamoto mbali mbali ikiwa ni pamoja na uwezo mdogo wa kujiendeleza elimu ya juu kwa wasichana, vitendo vya uzalilishaji, kukosa fursa ya kumiliki ardhi na uchereweshaji wa kesi zinapopelekwa mahakamani.

Aliwaomba Viongozi waunge mkono katika kuleta maendeleo endelevu katika jamii na kuwapa dhamana wanawake katika ngazi mbali mbali kwa kuzingatia uwiano wa ajira.

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba Mhe:Mwanajuma Majid Abdalla
akikabidhi cheki ya shilingi Milioni 1,500,000/= kwa kiongozi wa kikundi
 cha Duka Asha Mwalimu Haji, maara baada ya maadhimisho ya
siku ya wanawake Duniani.
Mkuu wa Wilaya ya Chake Chake Mhe:Hanuna Ibrahim Masoud akizungumza na
 wananchi wa wilaya ya Chake Chake katika maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani, 
kisiwani Pemba yaliyofanyika katika Uwanja wa MIchezo Gombani

0 comments:

Post a Comment