February 12, 2016

Kampuni ya simu Zantel, imeendelea kuipa msukumo sekta ya elimu Zanzibar, mara hii ikitoa msaada wa shilingi milioni kumi kwa Shirika la Huduma za Maktaba Zanzibar kwa ajili ya kununulia vitabu na uendeshaji wa shughuli zake.
Akizungumza katika hafla iliyofanyika leo katika jengo la maktaba hiyo Maisara mjini Zanzibar, Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo Benoit Janin, amesema msaada huo unalenga kusaidia upatikanaji wa maarifa miongoni mwa jamii ya Wazanzibari.
Janin amesema, ni miongoni mwa majukumu na wajibu wa Zantel, kuhakikisha inatoa huduma bora na zenye ufanisi zinazokidhi mahitaji ya wakaazi wanaoishi mijini na vijijini na kurahisisha upatikanaji wa taarifa za elimu, habari, utamaduni na burudani.
“Upatikanaji wa maarifa kwa wanajamii ni jambo la muhimu na suluhisho la changamoto hii ni kuhakikisha tunatoa fursa sawa kwa kuwezesha kukua kwa maktaba za jamii,” amesema Janin.
Aidha ameeleza kuwa, ni fahari kwa kampuni yao kusaidiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kuchangia ukuaji na ustawi wa jamii.
“Tunaamini kwamba kujifunza ni muhimu kwa maendeleo ya elimu kama moja maeneo ya shughuli zake za kusaidia jamii,” ameeleza Ofisa huyo.
Akitoa shukurani zake kwa Zantel, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Abdalla Mzee, ameipongeza kampuni hiyo kwa mchango wao wa miaka mingi katika kukuza maendeleo ya elimu Zanzibar.
“Tunafarijika na mchango wa Zantel katika kusaidia maendeleo ya elimu nchini, na msaada huu uliotolewa leo kwa maktaba yetu kuu utasaidia kurahisisha upatikanaji wa vitabu na hivyo kuimarisha mazingira ya utoaji maarifa miongoni mwa Wazanzibari,” ameeleza.
Hata hivyo, ameiomba kampuni hiyo kuangalia uwezekano wa kusaidia maeneo mengine ya kielimu yanayokabiliwa na changamoto kadhaa, ikiwemo kukamilisha ujenzi wa baadhi ya madarasa uliokwama, pamoja na madawati.
Mapema, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Huduma za Maktaba Zanzibar Sichana Mussa Foum, ameishukuru Zantel kwa msaada huo, akisema ni muhimu kwa wateja wa maktaba zake Unguja na Pemba.  
Amefahamisha kuwa, pamoja na jitihada za serikali kuziendeleza maktaba hizo, mchango wa taasisi nyengine unahitajika kutoana na ongezeko la wanafunzi na wananchi wanaohitaji huduma za maktaba. 



:Maelezo

0 comments:

Post a Comment