February 05, 2016

Waziri wa nchi afisi ya Rais Ikulu zanzibar Dk. Mwinyihaji Mkame Mwadini juzi usiku alikuwa ni miongoni mwa mamia ya Waandishi wa habari na wadau wa sekta ya habari Zanzibar katika maziko ya aliyekua mwandishi na mtangazaji wa vituo mbali mbali vya redio mjini Zanzibar Hafidh Hussein Mwinyi.
Hafidh maarufu Mpita Njia alifikwa na mauti katika maeneo ya Maungani, wilaya ya Magharibi B Unguja baada ya kupata ajali ya barabarani iliyohusisha vespa aliyokuwa akisafiria yeye na mpiga picha wa Idara ya Habari Maelezo Zanzibar Makame Mshenga na lori la mizigo lililokua likitokea mjini kuelekea maeneo ya Dimani.
Katibu wa klabu ya waandishi wa habari Zanzibar Faki Mjaka amesema msiba huo ni tukio la kushitua linalopaswa kuwa na mazingatio makubwa kwa kila mwanadamu.
“Sio ZPC (klabu ya waandishi wa habari Zanzibar) au familia pekee iliyoondokewa bali kila mmoja miongoni mwa wapenda haki kwani marehemu alikuwa akiipenda kazi yake kiasi wengi walikuwa wakimtabiria kuwa angekuwa miongoni mwa wanaharakati wakubwa watakaoikomboa jamii kupitia fani ya habari”, amesema Mjaka.
Nae mtangazaji wa kituo cha redio cha Coconut fm alichokuwa akifanyia kazi katika kipindi cha coco jambo, anne Julius alikitaja kifo cha hafidhi kuwa ni pigo na pengo litakalochukua muda mrefu kuzibika maoni yaliyoungwa mkono na mwandishi mwengine Tabia Makame.
“Tulimtegemea kwa uwezo alionao katika kujenga na kutetea hoja lakini pia ubunifu wake katika utekelezaji wa majukumu yake, hakika ni pigo kwa kituo lakini mimi nadhani kifo hiki kimenigusa zaidi kutokana na kuwa nilikuwa namtegemea zaidi katika kufanya kipindi chetu kuwa bora”, amesema anne kwa huzuni kubwa.
Nae mwandishi wa habari mwandamizi na mkufunzi wa mambo ya vyombo vya habari Ali Sultani aliandika katika ukurasa wa ‘face book’ kuwa licha ya kukutana nae kwa mara ya kwanza katika mkutano wa kujadili changamoto zinazowakabili waandishi wa habari na vyombo vya habari wakati wa uchaguzi mchana wa Alhamis muda mchache kabla ya kifo chake, amesema aligundua kuwa mwandishi huyo alikuwa na kipaji na uwezo mkubwa wa kiuandishi.
“Awali sikuwa namjua kabla ya kukutana nae leo(juzi) mchana kabla kukutwa na umauti, niligundua uwezo na kipaji ambacho kingelimfikisha mbali katika fani hii”, ameeleza mkongwe huyo ambaye alikuwa ni miongoni mwa watoa mada katika mkutano huo ulioandaliwa na shirika la Inter News.
Mbali na kituo hicho Hafidh kwa wakati tofauti alikuwa akifanya kazi katika vituo vya redio vya Adhana FM na Mwenge FM ambapo pia alikuwa ni mwalimu wa fani ya uandishi wa habari katika taasisi ya Mwenge Community Center inayomiliki kituo hicho cha redio.
Maziko hayo ya marehemu yaliyofanyika katika makaburi ya mwanakwerekwe yanatajwa kuwa ni ya kipekee kutokana na kuhudhuriwa na idadi kubwa ya watu licha kukamilika majira ya saa saba usiku kutokna na mwili wa marehemu kuharibika vibaya kichwani baada ya madaktari wa Hospitali ya Mnazi mmoja kushauri maiti hiyo izikwe kutokana na kukosekana kwa mtambo wa ubaridi katika chumba cha kuhifadhia maiti.

Wizara ya Uwezeshaji Ustawi wa Jamii, vijana wanawake na watoto, imetoa mkono wa pole kwa wanafamilia wote pamoja na wanahabari kwa msiba huo na kuwaomba kuwa na subra wakati wote wakuomboleza.
Katika taarifa yake imesema imepokea kwa masikitiko na mshtuko  taarifa ya kifo cha mwanahabari Hafidh Hussein Mwinyi kwa kuwa alikuwa mmoja kati ya wadau wa Wizara hiyo katika harakati za mapambano dhidi ya udhalilishaji wa wanawake na watoto Zanzibar.
Marehemu Hafidh alyezaliwa Februari 16, 1986 alipata elimu yake ya masingi na sekondari katika skuli ya Mwanakwerekwe C Unguja kabla ya kujiunga na Mwenge Community Center (MCC) kwa masomo ya uandishi wa habari katika ngazi ya cheti mwaka 2012 na akanza  kufanya kazi katika kituo cha redio cha Adhana FM na baadae Coconut FM, alifanya vipindi maalum katika radio ya Mwenge FM na alikuwa mwanachama wa klabu ya waandishi wa habari Zanzibar ZPC mwaka 2012.

MUNGU AMLAZE MAHALI PEMA PEPONI AMIN

0 comments:

Post a Comment