February 22, 2016

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

Zanzibar                                                                                                                    22 Februari, 2016

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Vijana wa Chama cha Mapinduzi (CCM)wametakiwa kujidhatiti zaidi kulinda na kuendeleza Mapinduzi ya mwaka 1964 na muungano uliozaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Wito huo umetolewa leo na Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein wakati alipokuwa akizungumza na viongozi wa Umoja wa Vijana wa chama hicho (UVCCM) mkoa wa kichama wa Mjini Unguja.
Alibainisha kuwa kuyalinda na kuyadumisha Mapinduzi na Muungano ni kulinda na kuendeleza amani na utulivu nchini hivyo vijana hilo ndilo jukumu lao la msingi kama warithi wa taifa.
“hakuna mbadala wa Mapinduzi, hakuna mbadala wa Muungano wala hakuna mbadala wa amani na utulivu wa nchi yetu hivyo ni lazima vijana mchukue nafasi yenu kulinda misingi hiyo ya nchi yetu” alisisistiza Dk. Shein
Alisema ni wakati wao vijana wa sasa kuchukua majukumu hao kwa kuwa hata wao “walikuwa vijana kama nyinyi na tulihimizwa kufanya hayo hayo na viongozi wetu na ndio maana tumefanikiwa kukabidhiwa uongozi wa nchi yetu” Dk. Shein aliwaeleza viongozi hao wa vijana kuanzia ngazi ya matawi hadi mkoa.
Aliongeza kuwa ni lazima vijana wazingatie “historia ya ukombozi wa nchi yenu na ya uongozi wake ndio mtaweza kuwa viongozi wazuri na tegemeo la maendeleo ya nchi yenu”
Dk. Shein ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliongeza kuwa vijana ni lazima wasome na kukumbushana mara kwa mara historia  ya mapambano ya Uhuru wa Zanzibar kwa kuwa ni muhimu katika kujenga mustakbala wa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katika hotuba yake hiyo kwa vijana hao, Dk. Shein alisisitiza kuimarisha umoja, maelewano na mshikamano miongoni mwa vijana na kubainisha kuwa huo ndio msingi mkubwa wa mafanikio sio tu katika kutekeleza majukumu yao katika chama bali pia katika kulijenga taifa.
Alihimiza vijana kujiepusha na vitendo vinavyoweza kusababisha uvunjaji wa amani na utulivu na kuwataka vijana kuhakikisha wanakuwa mstari wa mbele kutetea na kulinda amani na utulivu nchini.
Mkutano huo ambao ulifanyika katika ukumbi wa mikutano wa CCM mkoa wa mjini huko Amani ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa CCM hicho wakiwemo wajumbe wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) wa chama hicho.

0 comments:

Post a Comment