Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir ametia saini
mkataba wa nchi yake kujiunga rasmi kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Rais Kiir ametia saini mkataba huo jijini Dar
es Salaam mbele ya mwenyeji wake, Rais wa Tanzania John Magufuli, ambaye kwa
sasa ndiye mwenyekiti wa jumuiya hiyo.
Viongozi wa nchi za jumuiya hiyo waliidhinisha
kukubaliwa kwa Sudan Kusini kujiunga na jumuiya hiyo kwenye mkutano mkuu
uliofanyika mjini Arusha mwezi uliopita.
Sudan Kusini itakuwa nchi ya sita kujiunga na
jumuiya hiyo iliyoanza kwa nchi tatu Tanzania, Kenya na Uganda. Rwanda na
Burundi zilijiunga na jumuiya hiyo baadaye.
Baada ya kujiunga rasmi leo, Sudan Kusini
inatarajiwa kufungua mipaka yake kwa ajili ya biashara. Tayari kampuni na asasi
nyingi za kifedha kutoka Kenya zimefungua biashara nchini Sudan Kusini.
Wengi wanatarajia hatua ya leo itafungua fursa
zaidi za kibiashara kati ya Sudan Kusini na nchi wanachama wa jumuiya.
Wadadisi wengine wanaamini kuwa baadhi ya
miradi ambayo Sudan Kusini ingetaka kujumuishwa katika Jumuiya ya Afrika
Mashariki ni miundo msingi ikiwemo reli na mabomba ya mafuta.
0 comments:
Post a Comment