April 15, 2016

Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzaia Dkt. Rufaro Chatora amezishauri taasisi za Serikali, taasisi za kiraia na watu  binafsi kila mmoja kutekeleza wajibu wake katika kukabiliana na maradhi ya kipindupindu nchini.
Amesema maradhi ya kipindupindu yanapotokea katika nchi moja yanagusa nchi nyingi duniani kutokana na watu kusafiri kutoka nchi moja kwenda nyengine katika harakati zao za maisha.
Dkt. Chatora ameeleza hayo alipokuwa akizungumza katika mkutano na watendaji wakuu wa Wizara ya Afya na waandishi wa Habari katika ziara yake ya kuangalia hali ya maradhi ya kipindupindu Zanzibar tokea yalipoanza mwezi Septemba mwaka jana hadi hivi sasa ambapo  watu 2703 wamepata ugonjwa  huo.
Amesema maradhi ya kipindupindu ni rahisi kutibika iwapo kila mtu atatimiza wajibu wake na kufuata ushauri wa wataalamu wa afya ikiwa ni pamoja na kuacha  kutumia maji yasiyo salama ambayo ni moja ya chanzo kikubwa cha kupata maradhi hayo.
Mwakilishi huyo wa WHO amesema Shirika hilo kwa kushirikiana na mashirika mengine ya Kimataifa litaendelea kuunga mkono juhudi za  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kukabiliana na maradhi hayo ili kuhakikisha yanamalizika.
Akieleza hali ya kipindupindu ilivyo hivi sasa Zanzibar katika mkutano huo uliofanyika Wizara ya Afya Mnazimmoja, Mkurugenzi Kinga na ELimu ya Afya Dkt. Mohd Dahoma amesema hali bado sio nzuri na wanaendelea kupokea wagonjwa wengi katika kambi ya Chumbuni.
“Tunapokea  wagonjwa kati ya  10 hadi 15 kwa siku katika kambi ya Chumbuni, kwa bahati mbaya jana tulipokea wagonjwa 20  na kambi moja mpya imefunguliwa  katika kisiwa cha Tumbatu,’’ alisema Dkt. Dahoma.
Amesema jumla ya Kambi 17 za wagonjwa wa kipindupindu zimefunguliwa katika maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba na kumi kati yao zimefungwa baada ya kukosa mgonjwa wa maradhi hayo.
Ameongeza kuwa kati ya wagonjwa 2703 waliogunduliwa na maradhi hayo 34 wamefariki ikiwa ni  sawa na asilimia 1.3 na vijana wenye umri kuanzia miaka 17 ndio walioathirika zaidi.
Dkt. Dahoma amesema kisiwa cha Unguja kimekuwa na wagonjwa wengi  zaidi wa kipindupindu  asilimia 52.3 na Pemba ni asilimia 47.3 huku Mkoa Mjini Magharibi ukiongoza ukifuatiwa na Mkoa Kaskazini Pemba.
Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya amewashauri wananchi kuwawahisha  mapema vituo vya afya  watu wanaobainika na  dalili za maradhi ya kipindupindu kwa vile imeonekana wagonjwa wengi wanapopelekwa vituoni afya zao zinakuwa mbaya na matibabu yanakuwa magumu.


Muakilishi wa Shirika la Afya Duniani WHO Dk, Rufaro Chatora
katikati akizungumza na Wakuu wa sekta mbalimbali katika
Wizara ya Afya Zanzibar kuhusiana na Maradhi ya Kipindupindu  Zanzibar.
Kushoto yake ni Muakilishi wa WHO aliopo Zanzibar  Dk, Ghirmay Andemichael
na kulia yake ni Katibu Mkuu wizara ya Afya Zanzibar
Mohd Saleh Jidawi.


MAELEZO Zanzibar        

0 comments:

Post a Comment